Zayd aitaka rekodi ya Bocco

Muktasari:

  • John Bocco alisajiliwa klabu ya Simba akitokea Azam FC . Nyota Zayd kwa sasa yumo kwenye mbio za ufungaji mabao Ligi Kuu akiwa amewekwa wavuni  mabao matano sawa na Ibrahimu Ajib, huku Eliud Ambokile akiwa kinara na mabao tisa.

STRAIKA wa Azam, Yahya Zayd ameweka wazi kutaka kuifikia rekodi ya John Bocco ambaye kwa sasa anacheza Simba.

Zayd alisema anatambua timu yao msimu huu imesajili mastraika wengi wa maana lakini ana uwezo wa kuwa Mfungaji Bbora wa Azam na hata ligi kwa jumla kulingana na nafasi ambayo atakuwa anapewa.

Alisema anatambua anacheza nafasi yenye mastraika wa maana wenye rekodi nzuri katika ligi lakini yupo tayari kupambana akiwa mazoezini ili kumuonesha uwezo wake Kocha Hans Pluijm na kumpa nafasi ya kucheza mechi nyingi.

“Siwezi kusema moja kwa moja kama naweza kuifikia rekodi hiyo lakini malengo yangu ni hayo endapo nitafunga kila mechi ili kupata hata nafasi ya kuwa mfungaji bora wa Azam au ligi kwa ujumla na hayo mengine yatafauta,” alisema Zayd.

Bocco mpaka anaondoka Azam alikuwa mfungaji bora wa muda wote akianza kufanya hivyo tangu ikiwa ligi daraja la kwanza.

Kwa sasa Zayd amefunga mabao matano msimu huu wakati msimu uliopita alifunga mabao tisa, matano katika ligi, matatu kwenye kombe la Shirikisho (FA) na lingine alifunga kombe la Mapinduzi.