Zahera: Kagere hawezi muziki wa Makambo

Muktasari:

Makambo, Kagere tangu mwanzo wa msimu wamekuwa wakishindana katika mbio za ufungaji bora kabla ya Mnyarwanda kumpiku Mkongo huyo.

Dar es Salaam. Pamoja na Meddie Kagere kuongoza kwa kufunga mabao 23, lakini kocha Yanga, Mwinyi Zahera amesema mfunguji bora wake ni mshambuliaji Herietir Makambo.

Kagere amefunga mabao 23 na kuisaidia Simba kutwaa ubingwa huku Makambo akizifumania nyavu mara 17 katika msimu wa kwanza wa washambuliaji hao.

Zahera alisema sababu za kumpa ufungaji bora Makambo ni kutokana na kufunga mabao ya jitihada zake binafsi huku akimponda Kagere kuwa mabao yake mengi amefunga kwa mkwaju wa penalti.

"Makambo mbali na mabao hayo 17 aliyonayo hadi sasa pia alifunga mabao 6 yaliyokataliwa na waamuzi na hakuna bao hata moja ambao amefunga kwa mkwaju wa penalti kama ilivyo kwa Kagere anayetazamwa kama mfungaji bora msimu huu," alisema Zahera.

Wawili kumrithi Makambo

Wakati suala la Makambo kuondoka likiwa bado halijakamilika Zahera ametamba kushusha washambuliaji wawili makini na wenye ubora zaidi ya nyota huyo anayetajwa kutimka Yanga.

"Tayali nimeshafanya mazungumzo na washambuliaji wawili wa kigeni nadhani wanaweza kutua muda wowote lakini sitaki kuweka wazi kwasasa hadi hapo dili zao zitakapokamilika."

"Wakitua nchini na kumalizana na Yanga wanauwezo wa kufunga mabao 40 kila mmoja atafunga mabao 20 naamini uwezo wao natumaini wakimalizana na klabu wanaweza kuwa msaada na wanayanga wakasahau kabisa kwamba walikuwa na Makambo."

UONGOZI MPYA

Zahera ameupongeza uongozi mpya chini Mwenyekiti Mshindo Msola kuwa ameona mabadiliko makubwa kutoka kwao kwani wamekuwa wakimpa ushirikiano na kumshirikisha katika masuala yanayohusu soka.