Yanga Princess yaisaka Simba Queens

Muktasari:

Sio Mapinduzi tu isikuwa na pointi, bali haya Baobab Queens ya Dodoma na wageni wa ligi hiyo, Tanzanite ya Arusha nazo hazijaosha ushindi wala sare, lakini zikitofautiana uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa na waburuza mkia.

MWANDISHI WETU
MALIKIA wa Jangwani, Yanga Princess inayoshiriki Ligi Kuu ya Soka ya Wanawake (WPL) jioni hii imepata ushindi wake wa pili katika ligi hiyo kwa kuifunga Tanzanite FC ya Arusha na kuanza mbio za kuwafukuza watani zao Simba Queens waliopo juu yao.
Kwa ushindi huo wa jioni ya leo umeifanya Princess iliyoianza ligi hiyo vibaya kwa kufungwa bao 1-0 na Sisterz FC kutoka Kigoma, kufikisha alama sita baada ya mechi tatu na kuchumpa toka nafasi ya tisa hadi ya sita katika ligi inayoshirikisha timu 12.
Yanga Princess wametangishwa na watani wao wa jadi Simba Queens kwa tofauti ya alama moja tu, ikiwa nafasi ya tatu ikilingana alama sawa na Mlandizi Queens na Sisterz ambazo kila moja ina pointi 7.
Watetezi wa taji la ligi hiyom, JKT Queens ipo kileleni ikiwa ndio timu pekee ambayo imeshinda mechi zao zote kwa asilimia 100, ikifikisha alama 9 na mabao 31, huku wavu wake ukiwa haujaguswa kama ilivyo kwa Mlandizi na Sisterz.
Mkiani mwa msimamo wa ligi hiyo inayochezwa kwa msimu wa tatu mfululizo tangu ilipoasisiwa enzi za utawala wa TFF ya Jamal Malinzi,  wapo Mapinduzi Queens ambayo ndio timu pekee ambayo haijafunga bao hata moja, huku yenyewe ikiruhusu 29 kutokana na michezo mitatu ambayo yote imepoteza.
Sio Mapinduzi tu isikuwa na pointi, bali haya Baobab Queens ya Dodoma na wageni wa ligi hiyo, Tanzanite ya Arusha nazo hazijaosha ushindi wala sare, lakini zikitofautiana uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa na waburuza mkia.
Baobab wanashika nafasi ya 11 ikifunga bao moja na kufungwa 12, huku Tanzanite wakiwa juu yao ikiwa imefunga mabao mawili na kufungwa 10 na kumpa kazi Kocha aliyepandisha daraja, Abdallah Juma kuwa na kazi ya ziada kuizoea ligi hiyo.
Tanzanite ilipanda msimu huu baada ya kushika nafasi ya pili katika Ligi Daraja la Kwanza kwa kufungwa katika fainali ya ligi hiyo na Yanga Princess iliyoshiriki pia ligi ya daraja la kwanza kwa mara ya kwanza na kupanda ikiishangaza wazoefu hao.