Yanga Dodoma wakana kwenda mahakamani

Muktasari:

Kauli hiyo imetokana na taarifa ya Mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi ya Shirikisho la Soka nchini (TFF),Ally Mchungahela kuhusu wanachama walioenda kupinga uchaguzi huo mahakamani.

Dodoma. Sisi Dodoma? Ni swali la Mwenyekiti wa tawi la wanachama wa Yanga Dodoma,Fred Mushi akishangazwa na taarifa za tawi lao kutajwa kwenda mahakamani kupinga uchaguzi.
Mushi amedai kuwa tawi lao la Dodoma analoliongoza halijapinga uchaguzi huo mahakamani kama ilivyodaiwa zaidi ya kushangaa kusikia taarifa hizo.
"Hakuna kitu hicho tawi letu hatujaenda mahakamani kupinga uchaguzi huo kama taarifa iliyosemwa hivyo tunakanusha vikali na hatujui chochote kuhusu hilo zaidi ya kutaka uchaguzi ufanyike".Amesema Mushi
Katika hatua nyingine Mwenyekiti huyo ameweka wazi kuwa wanafuatilia jambo hilo na endapo watabaini kuhusika kwa wanachama wao bila kuwashirikisha uongozi watawachukulia hatua kali wanachama husika.
"Endapo tutabaini kuna wanachama wetu waliohusika kwenda mahakamani bila kutushirikisha tutawachukulia hatua kali sana".Amesisitiza Mwenyekiti huyo