Ya Mourinho yaanza kumkuta Ole Gunnar alia nyota wake

Muktasari:

  • Ripoti zinadai kwamba Solskjaer amewaweka kitimoto wachezaji wake na kuwaaambia kwamba hawakujituma kwa asilimia 100 katika mechi yao dhidi ya Barcelona

Manchester, England. Haya kimenuka tena huko Manchester United. Yaliyomkuta Jose Mourinho kwa wachezaji wanaelekea kumkuta Ole Gunnar Solskjaer baada ya kocha huyo kudai kwamba wachezaji wake hawajitumi baada ya kukumbana na kipigo kutoka kwa Barcelona kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Solskjaer amedai kwamba wachezaji wake hawakucheza kwa kujituma kwa asilimia 100 wakati walipokumbana na kipigo cha kudhalilisha cha jumla ya mabao 4-0 kwenye mechi zao mbili za hatua ya robo fainali katika michuano hiyo ya Ulaya.

Man United walichapwa 3-0 huko Nou Camp Jumanne iliyopita ikiwa ni wiki moja tangu walipokung'utwa 1-0 uwanjani Old Trafford na wababe hao wa Hispania.

Ripoti zinadai kwamba Solskjaer amewaweka kitimoto wachezaji wake na kuwaaambia kwamba hawakujituma kwa asilimia 100 katika mechi yao dhidi ya Barcelona hasa ile ya marudiano ambapo Lionel Messi alifunga mara mbili kwa mabao yaliyotokana na uzembe wa mabeki wa wababe hao wa Old Trafford.

Hicho kilikuwa kipigo cha tano katika mechi sana za karibuni na ndio maana jambo hilo limemfanya kocha Solskjaer kuwafokea wachezaji wake kwa kusema hawakucheza katika viwango vinavyohitajika na Man United.

Solskjaer ameweka wazi kwamba atalazimika kupitisha fagio na kufanya usajili mpya mwishoni mwa msimu huu huku akiwaambia wachezaji wake mwamba kama hawatapata matokeo ya ushindi kesho Jumapili huko nyumbani kwa Everton, Goodison Park basi wasahau kuhusu Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao.