Wema apelekwa mahabusu

Muktasari:

  • Amri ya kumkamata msanii huyo ilitolewa Juni 11, mwaka huu na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Maira Kasonde, baada ya mrembo huyo kushindwa kufika mahakamani hapo kwa ajili ya usikilizwaji wa kesi inayomkabili, wala mdhamini wake.

Dar es Salaam. Mwigizaji wa filamu Wema Sepetu ametupwa mahabusu baada ya kukamatwa kwa amri ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Wema amekamatwa  leo Jumatatu, Juni 17, 2017, baada ya kujisalimisha mahakamani hapo siku sita baada ya mahakama hiyo kutoa amri na hati ya kumkamata kwa kushindwa kufika kwenye kesi yake inayomkabili mahakamani hapo.

Mshindi huyo wa mashindano ya urembo nchini (Miss Tanzania 2006), amepandishwa katika gari la Magereza mchana huu na kupelekwa mahabusu katika gereza la Segerea hadi Juni 24, mwaka huu mahakama hiyo itakapotoa uamuzi wa ama kufutia dhamana au la.

Amri ya kumkamata msanii huyo ilitolewa Juni 11, mwaka huu na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Maira Kasonde, baada ya mrembo huyo kushindwa kufika mahakamani hapo kwa ajili ya usikilizwaji wa kesi inayomkabili, wala mdhamini wake.

Wema anakabiliwa na kesi ya jinai akikabiliwa na shtaka moja la kuchapisha video ya ngono na kusambaza katika mtandao  wa kijamii wa Instagram.