Wawili waenguliwa mechi ya Simba

Muktasari:

  • Meneja wa timu hiyo, Faraji Muya alisema wamefanya maandalizi ya kutosha na Simba wasitarajie mteremko kwani lengo lao ni pointi tatu ili kujiweka nafasi nzuri kwenye msimamo.

MWANZA. KMC itawakosa nyota wawili Charles Ilanfya na Emanuel Mvuyekure ambao ni wagonjwa, huku wengine wapo fiti kuikabili Simba kesho Alhamisi na wametamba kuibuka na ushindi.

KMC inaingia uwanjani ikiwa imekusanya pointi 42 baada ya kucheza mechi 32 ikishika nafasi ya saba na inaikaribisha Simba Uwanja wa CCM Kirumba jijini hapa.

Timu zote mbili ni za jijini Dra es Salaam lakini KMC inatumia uwanja huo kama uwanja wa nyumbani baada ya kuhama Uwanja Uhuru ambao unatumika kwa ajili ya michuano ya AFCON U17 wakati Simba uwanja wa nyumbani kwasasa ni Jamhuri mkoani Morogoro.

Meneja wa timu hiyo, Faraji Muya alisema wamefanya maandalizi ya kutosha na Simba wasitarajie mteremko kwani lengo lao ni pointi tatu ili kujiweka nafasi nzuri kwenye msimamo.

“Wote wanasumbuliwa na malaria lakini wengine wana ari na morari nzuri, tunachotaka ni pointi tatu bila kujali tunacheza na timu gani isipokuwa tunaenda kupambana,” alisema Muya.

Meneja huyo aliongeza, pamoja na mchezo huo kuwa mgumu lakini watakuwa makini kutoruhusu mashambulizi langoni mwao na wanataka kuondoa uteja kwa wapinzani hao kutokana kufungwa mechi ya raundi ya kwanza. Alisema hawaiogopi Simba na wanaiona kama timu nyingine ya kawaida Ligi Kuu hivyo wanashuka uwanjani wakisaka ushindi na kukiri wazi ligi ni ngumu na kila mmoja anapambana kivyake.