Wanariadha Dar es Salaam kugombea elfu 50

Muktasari:

  • Dar es Salaam imekuwa ikifanya vizuri katika riadha hasa kwenye mbio fupi na za kati katika mashindano ya Taifa.

Dar es Salaam.Wanariadha wa mkoa wa Dar es Salam watapimana uwezo katika mashindano ya uwanjani ya ‘Mzizima Track and Field Championship’ Jumapili mshindi ataondoka na Sh50,000.

Mashindano hayo yatafanyika kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam yakilenga kuchagua timu itakayoiwakilisha Dar es Salaam kwenye mashindano ya Taifa Juali 5, Arusha.

Katibu wa riadha Dar es Salaam (DAAA), Kapteni mstaafu Lucas Nkungu, amesema mashindano hayo yameandaliwa na kufadhiliwa na Nyange Mtoro ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa chama hicho.

Amesema mashindano hayo yanalenga kuibua vipaji na kuhamasisha mbio za uwanjani, lakini pia kuchagua timu ya mkoa kwa ajili ya mashindano ya Taifa.

Amesema yatashirikisha mbio za uwanjani (mita 100 mpaka 10000) mitupo (Kurusha Tufe, Kisahani na Mkuki), sanjari na michezo ya miruko mitatu (tripple jump) na Kuruka Chini (long jump).

Amesema washindi watazawadiwa zawadi za fedha bingwa ataondoka na Sh50,000 wa pili 30,000 na wa tatu 20,000 na pia baadhi yao wataingia katika timu ya Mkoa tayari kwa mashindano ya Taifa.

Alitoa wito kwa klabu, shule na washiriki binafsi kujitokeza kwa wingi kushiriki kwani ni bure hakuna kiingilio.