Wametobolewa! Bandari FC yavuruga rekodi ya Gor Mahia

Muktasari:

  • Gor Mahia kabla ya mchezo huo ilikuwa na rekodi ya kucheza takribani mechi 28 bila kufungwa

Nairobi, Kenya. Hatimaye utabiri kuwa Agosti utakuwa mwezi wa majanga kwa mabingwa watetezi wa KPL, Gor Mahia, umeanza kuonekana baada ya rekodi ya kucheza bila kutobolewa kuvurugwa na Bandari FC kwa kipigo cha mabao 2-1, kule Mbaraki, Mombasa.

Gor Mahia iliingia uwanjani ikiwa na morali kubwa hasa baada ya kucheza takribani mechi 28 bila kufungwa ikiwa ni mechi 22 za KPL msimu huu na tatu za kimataifa. Walikuwa ndio wanaume mjini kabla mabao ya Dan Guya katika dakika 11, na Yema Mwana (dakika 34) hayajavuruga vichwa vyao katika kipindi cha kwanza.

Hadi kipindi cha kwanza kinamalizika, Kogalo walikuwa hoi. Hawakuamini kilichotokea, ubao wa matokeo ulikuwa unasomeka 2-0. Wakarudi uwanjani katika kipindi wakiwa na hasira balaa, ambapo kunako dakika ya 77, Jacques Tuyisenge alizamisha bao la kufutia machozi.

Katika mchezo huo mkali wa kusisimua ambao ni wa kwanza kwa Kogali kupoteza msimu huu, ulimshuhudia kipa wa Bandari, Farouk Shikhalo, ambaye hajafungwa akisimama kidete kuwazuia mabingwa hao mara 16 wa KPL, katika sehemu kubwa ya mchezo, akipangua michomo kadhaa katika kipindi cha pili. Mwisho wa siku Bandari 2-1 Gor Mahia.

Kwa matokeo hayo Bandari, ambao walishuhudia nyota wao, Fred Nkata akioneshwa kadi nyekundu katika dakika 10 za mwisho wa mchezo, wanakwea hadi nafasi ya pili ya msimamo wa ligi, wakiwa wamefikisha pointi 45, pointi 11 nyuma ya Gor Mahia wanaongoza wakiwa na alama zao 56 na mechi tatu mkononi.

Kikosi cha Bandari FC:

Farouk Shikalo (Kipa), Nicholas Meja, Fred Nkata, Bernard Odhiambo, Felly Mulumba, Dan Guya, Joshua Oyoo, Willy Lugogo, Wycliffe Ochomo, Yema Mwana and Darius Msagha. 

Akiba: Joseph Elimlim, Dan Otewa, Siraj Mohammed, Keegan Ndemi, Benjamin Mosha, Shaban Kenga and Hamisi Abdalah. 

Kikosi cha Gor Mahia:

Shaban Odhoji, Godfrey Walusimbi, Harun Shakava, Joash Onyango, Philemon Otieno, Ernest Wendo, Humphrey Mieno, Francis Kahata, George Odhiambo, Jacques Tuyisnege, Francis Mustapha.

Akiba: Peter Odhiambo, Charles Momanyi, Kevin Omondi, Lawrence Juma, Ephrem Guikan, Bernard Ondiek, Innocent Wafula.