Walivyoponzwa na unga hatari!

Muktasari:

Heshima ya staa wa zamani wa soka duniani, Diego Maradona
hakuna asiyeijua kutokana na kufanya kwake makubwa ambayo kila mtu hakuna anayebisha kuhusu ubora wake.

UKIJIINGIZA tu kwenye hizi mambo umekwisha. Siku chache zilizopita kiungo mpya wa Yanga, Mohammed Issa 'Banka ' alifungiwa miezi 14 baada ya kukutwa na hatia ya kutumia dawa ambazo haziruhusiwi michezoni.
Zipo dawa za aina nyingi ambazo wakikubaini wenye mpira wao umekwisha, tusiandikie mate wakati wino upo mwanangu wafuatao ni wanasoka wakubwa duniani ambao yaliwakuta na wakakutana na vifungo tofauti vya soka.

Edgar Davids
Kwasasa amestaafu akiwa ametoka kuachana na klabu moja ya ligi daraja la chini maarufu iliyokuwa ikiitwa Barner, enzi za soka lake mwaka 2001 akiwa mchezaji wa Juventus aliwai kukutwa na shtaka la kutumia madawa ya kulevya.
Hukumua yake ilikuwa ni  adhabu ya kukaa nje ya soka kwa miezi 16, adhabu ambayo ingemfanya akose michuano ya Kombe la Dunia mwaka 2002. Lakini baadae alikata rufaa na kupunguziwa adhabu.

Jake Livermore
Alisajiliwa na Hull city akitokea Tottenham kwa dau la paundi milioni 8 na kumfanya kuwa mchezaji ghali katika historia ya klabu ya Hull city.
Lakini maisha ya soka hayakuwa vizuri kwake toka alipogundulika baada ya vipimo kwamba ni kweli anatumia madawa ya kulevya aina ya Cocaine.
Hii imemfanya kutokuwa na maisha marefu katika soka lake kama mchezaji wa kulipwa.

Stan Lazaridis
Akiwa na miaka 34 akiwa kwenye klabu ya Perth Glory ya nchini kwao Australia, alifungiwa kutoshiriki mchezo wa soka kwa miezi 12 kutokana na kugundulika kwamba ni kweli ni mtumiaji wa madawa ya kulevya.
Mara baada ya adhabu hiyo akaamua kustaafu kabisa soka kutokana na umri wake kufikia miaka 34.

Deco
Wengi huenda hawakulisikia hili la kumhusu kiungo aliyewai kung'aa na klabu za Barcelona na Chelsea lakini aliwai kuingia kwenye kashfa ya kutumia madawa ya kulevya mara baada ya kustaafu soka akiwa ana miaka 36 huko nchini Brazil kwenye klabu ya Fluminense.
Deco aliingia kwenye kashfa ya madawa  mara baada ya kustaafu soka lake lakini bado alikata rufaa nakudai kwamba upimaji ulifanyika kimakosa na haikuwa vipimo vya madawa ya kulevya.

Abel Xavier
Anakumbukwa vyema kwa kubadilisha sana mitindo ya nywele na ndevu lakini pia akiwa na sifa ya kati ya wanasoka waliozichezea klabu nyingi.
Lakini kashfa ya madawa ya kulevya ilimkuta akiwa na klabu ya West Ham mwaka 2005 hali iliyomfanya afungiwe kwa miezi 18.

Adrian Mutu
Nyota raia wa Romania aliingia kwenye kashfa ya kutumia madawa ya kulevya aina ya kokaine mwaka 2003 wakati alipokuwa akiichezea klabu ya Chelsea.
Alipigwa rungu na chama cha soka nchini Uingereza lakini pia akifungiwa kucheza soka kwa mwaka mzima. Mara baada ya hapo akawa hatulii na klabu moja uku akipambana kurejea kwenye kiwango chake.

Jermaine Hue
Ni mchezaji mstaafu raia wa Jamaica akikumbukwa haswa kwa mengi aliyoyafanya katika klabu alizozichezea na kuitumikia vyema timu yake ya taifa ya Jamaica.
Lakini alikumbwa na kashfa ya kutumia madawa ya kulevya na vipimo vilionyesha ni kweli ni mtumiaji wa madawa hayo wakati alipotoka kutumikia timu yake ya taifa kucheza mchezo wa kufudhu kushiriki Kombe la Dunia, wakicheza dhidi ya Honduras, kipindi iko akiwa ana miaka 35.
Alikutwa hatiani na kupewa adhabu iliyomgharimu kukaa nje kwa miezi 9.

Chris Armstrong
Akiwa ana miaka 23 tu mwaka 1995 aliingia kwenye kashfa ya kutumia madawa ya kulevya na alipofanyiwa vipimo vikaonyesha ni kweli alikuwa mtumiaji wa madawa ya kulevya na hapo aliweka rekodi mbaya ya kuwa mchezaji wa kwanza wa ligi kuu Uingereza kugkugundulika kwamba anatumia madawa ya kulevya.
 Lakini mara baada ya muda alirejea klabuni Crystal Palace lakini alirudi na majanga maana kurejea kwake uwanjani kukaishuhudia Crystal Palace ikishuka daraja kutoka Ligi kuu Uingereza mpaka ligi daraja la kwanza nchini humo.
Hilo halikumfanya asajiliwe na klabu ya Tottenham ambapo dau la usajili wake lilimfanya kuwa moja ya wachezaji waliosajiliwa kwa dau nono lakini pia kuwa mchezaji wa kwanza klabuni Crystal Palace kuuzwa kwa bei kubwa ya paundi milioni 4.5

Gerrard Kinsella
Aliwai kucheza pamoja na nyota wasasa wa Chelsea, Ross Barkley. Lakini huyu majanga yalimkuta mwaka 2013 akiwa anaitumikia klabu ya daraja la chini nchini Uingereza, klabu ya Fleetwood Town ambapo alipofanyiwa vipimo ilionekana ni kweli anatumia madawa ya kulevya.
 Mara baada ya hukumu yake ya kufungiwa miaka miwili kutokana na kugundulika ni kweli anatumia madawa ya kulevya kumalizika amekuwa akisaka timu ya kuichezea bila mafanikio.

Diego Maradona
Hakuna asiyejua ukubwa wake na heshima yake katika soka. Amefanya makubwa ambayo kila mtu hakuna anayebisha kuhusu ubora wake.
Lakini kashfa na kugundulika kwamba alikuwa anatumia madawa ya kulevya ndilo jambo ambalo kwa namna moja ama nyengine limemfanya asiwekwe ngazi moja na mfalme wa soka, Pele.
Kwa mara ya kwanza aligundulika kwamba anatumia madawa ya kulevya mwaka 1991 alipokuwa anaitumikia klabu ya Napoli ya nchini Italia na hukumu yake alihukumiwa adhabu ya miezi 15 hali iliyomfanya aamue kuachanana klabu hiyo na kujiunga na klabu ya Sevilla ya nchini Hispania.
Miaka mitatu baadae, yaani mwaka 1994 akiwa mchezaji wa klabu ya Newell's Old Boys alikutwa na hatia kwa mara nyengine tena kutokana na madawa ya kulevya hali iliyomfanya kucheza michezo miwili tu ya Kombe la Dunia mwaka huo wa 1994.