Vita ya mabondia Mabibo, Manzese yaanza upya

Muktasari:

Bondia Mfaume Mfaume ndiye aliibua vita ya mabondia wa maeneo hayo baada ya kuwachapa Habibu Pengo, Deo Samwel na hivi karibuni alimchapa Keis Ally.
Promota wa pambano hilo, Arteta Nyanda alisema maandalizi yamekamilika na pambano hilo litatanguliwa na mengine 15.

VITA ya mabondia wa kambi ya Mabibo na Manzese wanaonolewa na makocha, Rama Jaha na Christopher Mzazi imeibuka upya baada ya mabondia wa kambi hizo, Baina Mazola na Mastika the Don kusaini mkataba kuzuchapa kesho Jumamosi.

Mabondia hao ambao watapanda ulingoni kesho ukumbi wa Manyara Park, Tandale wameibua vita upya ya mabondia wa kambi hizo mbili zinazochuana kwenye masumbwi nchini.

Leo Ijumaa mashabiki wao walifurika kwenye viwanja vya Las Vegas, Mabibo kuwasapoti wakati wa kupima uzito na afya huku kila upande ukijinasibu kushinda.

Mazola anayenolewa na Mzazi wa Manzese alisema hatopenda kuwachosha mashabiki hivyo atahakikisha pambano linakwisha mapema.

Huku akishangiliwa na mamia ya mashabiki waliojitokeza katika zoezi hilo la awali kabla ya kupanda ulingoni, Mazola alisema kambi ya Mabibo imeingia anga tofauti safari hii.

Mpinzani wake ambaye jina lake halisi ni Muksini Swalehe alisema amejiandaa kuendeleza rekodi ya Mabibo.

"Kambi yetu ya Nakos haina kazi mbovu, tuko vizuri ndio sababu Manzese kila wanapokutana na sisi lazima wakae," alisema