Vishale mambo bado mazito

Picha na mtandao

Muktasari:

Akizungumza na Mwanaspoti jana, Makamu Mwenyekiti wa Tada, Redempta Mwebesa alisema mpaka sasa timu haijaingia kambini kutokana na ukata.

CHAMA cha Mchezo wa Vishale Tanzania (Tada), kimeiangukia serikali na wadau kikiomba Sh12 milioni kuiwezesha timu ya Taifa ya mchezo huo kushiriki mashindano nchini Uganda.

Mashindano hayo maarufu kama Uganda Open yataanza Septemba 13 hadi 15, mwaka huu na yatashirikisha nchi za Tanzania, Rwanda, Uganda na Kenya.

Akizungumza na Mwanaspoti jana, Makamu Mwenyekiti wa Tada, Redempta Mwebesa alisema mpaka sasa timu haijaingia kambini kutokana na ukata.

“Tulitaka iwe kambini kwa wiki tatu, lakini hadi sasa fedha imekuwa ngumu na bajeti yetu ni Sh14 milioni ambayo inahusisha kila kitu kuanzia kambi, chakula na malazi pamoja na kusafirisha timu.

“Kwa sasa tuna Sh2 milioni tu, hivyo tunahitaji msaada wa Sh12 milioni na ndio sababu tumeona tufikishe kilio chetu kwa wadau wa michezo na serikali ili Tanzania iweze kutetea ubingwa wake,” alisema Mwebesa.

Alisema ili kuwawezesha wachezaji kwenda kushiriki kikamilifu, kufanya vizuri na kutetea ubingwa ni lazima kuwepo na maandalizi ya uhakika na ya mapema.

Pia, Mwebesa alisema sio timu ya taifa tu inayoruhusiwa kushiriki mashindano hayo, bali hata klabu na mchezaji mmoja mmoja mwenye uwezo anaruhusiwa kushiriki.

Mchezo wa vishale umekuwa ukicheza mara nyingi katika sehemu za starehe.