Unaambiwa hivi, Neymar anasubiri ofa Real Madrid

Muktasari:

  • Neymar sasa anaona anapoteza tu muda kwenye timu hiyo na hivyo kufikiria kurudi Hispania ambako kuna timu siriazi kwenye kusaka mataji kwa kila msimu.

PARIS, UFARANSA.SUPASTAA wa Kibrazili, Neymar ameripotiwa anawasubiri tu Real Madrid wapeleke ofa ya kumchukua na hatasita kuipiga kibuti PSG.

Kwa mujibu wa taarifa za kutoka Hispania ni mchezaji huyo ameshapanga hadi mabegi yake akijiweka tayari kabisa kwa ajili ya kurejea kwenye La Liga.

Neymar amekuwa akihusishwa na mpango wa kurudi Hispania, lakini si kwenda kuichezea timu yake ya zamani ya Barcelona bali kujiunga na mahasimu wao, Real Madrid.

Ni miaka miwili tu imepita tangu PSG ilipovunja benchi kuweka rekodi duniani ya kutumia Pauni 198 milioni kunasa huduma ya mchezaji huyo.

PSG iliamini baada ya kumnasa Mbrazili huyo inaweza kushinda ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, lakini jambo hilo limeshindwa kutokea na msimu huu ilitupwa nje na timu dhaifu ya Manchester United katika hatua ya 16 bora.

Neymar sasa anaona anapoteza tu muda kwenye timu hiyo na hivyo kufikiria kurudi Hispania ambako kuna timu siriazi kwenye kusaka mataji kwa kila msimu.

Huko Real Madrid Kocha Zinedine Zidane amepanga kufanya usajili mkubwa wa mastaa wa maana na jambo hilo linamfanya Neymar kusubiri tu ofa akakipige.

Staa mwenzake wa PSG, Kylian Mbappe naye amekuwa akihusishwa na mpango wa kwenda kukipiga huko Bernabeu.

PSG ilimsajili Mbappe kwa Pauni 156 milioni mwaka juzi ilipomng’oa kutoka AS Monaco.