Ulimwengu aifanyia umafia Simba

Muktasari:

Simba inatarajiwa kuanza kutupa karata yake ya kwanza Januari 12  katika mchezo wao dhidi ya JS Saoura ambayo amejiunga nayo Mtanzania, Thomas Ulimwengu hivi karibuni akitokea Klabu ya Al Hilal nchini Sudan.

Dar es Salaam. Klabu ya Simba imezidishiwa ugumu katika mchezo wao wa Ligi ya Mabingwa  baada ya mshambuliaji Thomas Ulimwengu wa Taifa Stars na klabu JS Saoura kugoma kufichua aina ya mazoezi wanayofanya wakiwa katika maandalizi ya mechi yao.
Simba inatarajiwa kuanza kutupa karata yake ya kwanza Januari 12, wakiwa nyumbani katika mchezo wao dhidi ya JS Saoura ambayo siku za hivi karibu alijiunga nayo akitokea Al Hilal ya Sudan.
Ulimwengu amesema,  wanaiheshimu Simba lakini hawezi kuzungumza zaidi.
“Mechi itakuwa nzuri na tunawaheshimu wapinzani wetu, kikubwa ni kujitolea tu katika mchezo huu ili kuweza kupata matokeo mazuri kwa kufata maelekezo ya mwalimu,” alisema Ulimwengu.
Hata hivyo mshambuliaji huyo aligoma kusema aina gani ya maandalizi wanayofanya nchini Algeria kuelekea katika mchezo huo wa Ligi ya mabingwa, na kusema wanafanya maandalizi ya kawaida tu.
“Tunajiandaa kawaida tu kama michezo mingine kwa kufata program ya mwalimu, lakini kuna utofauti mkubwa sana kwenye soka kati ya Sudan na Algeria,” alisema.