Ukifanya kazi na Diamond, umetusua kimaisha

Muktasari:

  • Imeelezwa kwamba mwanamuziki wa kizazi kipya Diamond Platnumz amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha vijana wenzake anawainua vipaji vyao ni kiuchumi.

MWANAMUZIKI anayetikisa ndani na nje ya nchini, Nasibu Abdull 'Diamond Platnumz' amefanyika daraja kwa vijana wenzake kuwatoa kimaisha kama anavyofichua mcheza shoo wake Ahmed Makambi 'Dumy'.
Dumy amefunguka namna ambavyo Diamond Platnumz, amekuwa msaada wa kuinua vijana wenzake kwa kuwapa fursa ya kufanya nao kazi kwamba ni mfano wa kuigwa na wengine.
Anasema ameanza kufanya kazi na Diamond Platnumz tangu hajatoboa kimuziki mpaka sasa ambapo anajulikana ndani na nje ya nchini, akimuelezea kwamba ni kijana ambaye haridhiki na alichopata zaidi ya kutamani mafanikio makubwa zaidi.
"Nina hatua kubwa kimaisha kupitia kucheza shoo kwenye nyimbo za Diamond Platnumz na nyimbo ambayo ilianza kututoa sisi wacheza shoo ni ya 'Moyo' ambayo ilikuwa inachezeka.
"Ingawa hata ile ya Nenda Kamwambie tulikuwemo ndani lakini haikuwa ya kuchezeka sana, kifupi nyimbo zote za Diamond Platnumz nimecheza kuanzia ya kwanza mpaka hii ya Inama," anasema
Alipoulizwa kwamba ni changamoto ya aina gani kufanya kazi na staa huyo? Alijibu kuwa "Diamond Platnumz anapenda kazi bora, yeye mwenyewe anajituma akianza kufanya mazoezi unaweza ukashangaa, hivyo siwezi kuwa mvivu wa kupambana.
"Kwenye maisha ya kawaida ni kijana ambaye anajishusha na kushirikiana na kila mtu, tofauti na anavyoonekana akiwa kwenye steji, huyo ndiye Diamond ninayemfahamu mimi,"anasema.