Ujanja wa Zlatko waizima Mtibwa

Muktasari:

Yanga itacheza na Coastal Union katika mchezo ujao kwenye Uwanja wa Mkapa.

Morogoro. Vita ya ubingwa wa Ligi Kuu kwa vigogo imeanza kushika kasi baada ya Yanga nao kushinda katika mchezo wa jana wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Mtibwa Sugar.

Baada ya ushindi wa juzi wa Azam FC dhidi ya Tanzania Prisons na kufikisha pointi 12 kileleni mwa msimamo, mabingwa watetezi Simba nao waliichapa Gwambina 3-0 na kusogea hadi nafasi ya pili.

Azam FC ndiyo timu pekee ambayo imeshinda mechi zake zote nne kutokana na ushindi wa juzi wa bao 1-0 lililowekwa kimiani na Prince Dube, ambaye anaongoza katika ufungaji akiwa na mabao matatu.

Katika Uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro jana, mabingwa wa zamani, Yanga walipata ushindi wao wa tatu mfululizo kupitia kwa Lamine Moro, akimalizia kona safi ya kiungo wa kimataifa wa Angola, Carlinhos dakika ya 61.

Ushindi huo unaifanya Yanga kuwa na pointi 10, sawa na Simba, ambayo inashika nafasi ya piili katika msimamo kutokana na idadi ya mabao.

Kocha wa Yanga, Zlatko Krmpotic aliamua kuwavuruga Mtibwa kwa kumuanzisha Carlinhos, ambaye wengi walidhani kuwa ingekuwa ngumu kwa kiungo huyo kufanya maajabu kutokana na ubora wa Uwanja wa jamhuri.

Krmpotic aliamua kumuanzisha pembeni katika mfumo wa 4-2-3-1, akiwa katika eneo la juu pamoja na Mukoko Tonombe na Tuisila Kisinda, huku viungo wa chini yao wakibaki Feisal Salum na zawadi Mauya.

Yanga haikuwa na mabadiliko makubwa katika safu ya ulinzi, kwa kipa Metacha Mnatta alikuwa akilindwa na Kibwana Shomari, Yassin Mustapha, Lamine Moro na Bakari Mwamnyeto, wakati mshambuliaji pekee akiendelea kusimama Michael Sarpong.

Akili ya kocha huyo raia wa Serbia ilikuwa ni kumtumia zaidi Sarpong katika kulazimisha na kufanikiwa kuchezewa madhambi ili kuwa na mipira mingi iliyokufa kwa ajili ya kutengeneza mabao. Hilo lilionekana tangu kipindi cha kwanza licha ya mashabiki wengi kuona kama Carlinhos hakuwa na msaada katika mchezo wa wazi.

Kona ya dakika ya 61 ndiyo iliyotoa tofauti katika mchezo huo wanne katika kila timu, kwani Lamine alitulia zaidi katika kugeuza mguu na kuuelekeza mpira katika kona ya mbali ya lango.

Licha ya bao hilo kuwainua zaidi vijana wa kocha Zuberi Katwila, lakini eneo la katikati ambalo Mtibwa walimtumia Baraka Majogoro na Haruna Chanongo, ambalo lilizidiwa na utatu wa Mauya, Fei Toto na Mukoko.

Hilo lilimfanya Katwila kumtoa Majogoro ili kuongeza nguvu katika eneo hilo bila mafanikio.

Kocha msaidizi wa Yanga, Juma Mwambusi alikiri kufanya ujanja wa kuwashangaza Mtibwa kwa kumuanzisha Carlinhos, ambaye wengi walidhani atashindwa kuonyesha makali yake.

Yanga imemaliza mechi mbili za ugenini kwa kuvuna pointi sita na sasa inarudi Dar es Salaam kwa michezo mitatu ya nyumbani, ikianza na Coastal Union, kisha na Polisi Tanzania na Septemba 18 kuivaa Simba.

Katika mchezo mwingine wa jana, Mwadui iliibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Ihefu FC mkoani Shinyanga, wakati Ruvu Shooting wakilazimishwa suluhu na Biashara katika Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.