Uhuru anusa Ligi Kuu Afrika Kusini

Muktasari:

  • Akizungumzia uwezekano wa kupanda daraja, Uhuru alisema ni mkubwa na anachoshukuru Mungu ni kwamba amekuwa na maelewano mazuri na wachezaji wenzake.

HUENDA msimu ujao winga wa zamani wa Simba, Uhuru Seleman akacheza Ligi Kuu Afrika Kusini ‘PSL’ kutokana na chama lake la Royal Eagles kuwa kwenye nafasi nzuri ya kupanda daraja.

Uhuru alirejea nchini na kuichezea Biashara United ya Mara kwa miezi michache kabla ya kuamua kurudi tena Afrika Kusini ambako alikuwa akiichezea Mthatha Bucks.

Akizungumzia uwezekano wa kupanda daraja, Uhuru alisema ni mkubwa na anachoshukuru Mungu ni kwamba amekuwa na maelewano mazuri na wachezaji wenzake.

“Hii siyo mara yangu ya kwanza kuichezea Royal Eagles, kipindi kilichopita nilivurugana na kocha, kiujumla hapakuwa na amani kwenye klabu hivyo ikanilazimu kuondoka.

“Nimerejea na tupo kwenye kiwango kizuri na nimategemeo yangu kuwa tunapanda daraja,” alisema Uhuru.

Winga huyo ambaye Jumapili walikuwa na mchezo dhidi ya TS Galaxy, alisema katika mechi chache zilizosalia wamepanga kushinda ili wamalize kwenye nafasi ya kwanza.

“Tukimaliza kwenye nafasi hiyo ni moja kwa moja tunapanda daraja, lakini kinyume cha hapo tutacheza mchujo wa kuwania kupanda,” alisema Uhuru.

LIGI DARAJA LA KWANZA SAUZI

Timu MP W D L F A D P

1 Stellenbosch 27 14 7 6 40 20 +20 49

2 Ajax Cape Town 26 13 6 7 36 24 +12 45

3 Royal Eagles 26 12 8 6 35 20 +15 44

(kabla ya mechi za jana)