Uchaguzi Yanga moto! Mashabiki Dar kumuona Rais Magufuli

Muktasari:

  • Matawi ya Yanga Mkoa wa Dar es Salaam, wameazimia kwenda moja kwa moja kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli ili awasaidie kuhusiana na sintofahamu ya uchaguzi wao.

MATAWI ya Yanga Mkoa wa Dar es Salaam, wamemuomba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Magufuli kuwasaidia kuliambia Baraza la Michezo nchini (BMT), kuwaruhusu kufanya mkutano wa dharula.

Mratibu wa matawi hayo, Kaisi Edwin Mwasongwe amesema wanaamini mkutano huo ndio utatoa majibu ya sintofahamu inayoendelea kuhusiana na uchaguzi wa Yanga.

"Jambo la Yanga linamalizwa na Wanayanga wenyewe hakuna mtu wa kutoka nje kwamba ndiye atalimaliza ndio maana tunahitaji rais wa nchini atupe ruhusa ya kufanya mkutano wa dharula.

"Tunaamini Rais wetu Magufuli yupo kwa ajili ya wananchi wote kwa sababu ndio waliomchagua, maana tumechoka na propaganda ya wale ambao wapo kwenye dhamana ya mchezo hawatupi jibu sahihi zaidi ya kutusumbua na kuwaweka wanachama njia panda.

"Mbali na Baraza la michezo kutotoa majibu yaliosahihi pia wapo wanachama ambao wapo kwenye nyazifa za juu wanachangia kuidhoofisha, lakini pia wapo ambao wanajitokeza kwenye vyombo vya habari kuwachafua viongozi waliopo kwa wanakula pesa za michango ya wanachama, kitu hicho ni uongo,"anasema mratibu huyo.

Matawi ya Yanga Mkoa wa Dar es Salaam, wameazimia kwenda moja kwa moja kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli ili awasaidie kuhusiana na sintofahamu ya uchaguzi wao.