Twiga Stars kibaruani Congo

Muktasari:

  • Kocha Mkuu wa Twiga Stars, Bakari Shime alisema, baada ya kuwaona wapinzani wao katika mchezo huo hata kama watakuwa ugenini, watapambana na kushinda.

KIKOSI cha Timu ya Taifa ya Wanawake ya Tanzania ‘Twiga Stars’ leo Jumanne kitakuwa uwanjani kukipiga na DR Congo katika mchezo wa marudiano wa kuwania kufuzu fainali za Olimpiki zitakazofanyika mwakani kule Japan.

Twiga Stars iliyoanza safari ya kwenda Congo majuzi kwa ndege ya Shirika la Ethiopia ikipitia Addis Ababa, itacheza mchezo huo baada ya sare ya mabao 2-2 iliyoipata katika mechi ya awali iliyochezwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.

Kocha Mkuu wa Twiga Stars, Bakari Shime alisema, baada ya kuwaona wapinzani wao katika mchezo huo hata kama watakuwa ugenini, watapambana na kushinda.

“Tumejiandaa vizuri na tuko tayari kwa mchezo huo ambao bila shaka utakuwa mgumu kwetu kwa sababu Congo itakuwa nyumbani kuhakikisha inapata mataokeo mazuri. Ninachowaambia Watanzania watambue kuwa tutapambana na tutashinda. Kila kitu kwa upande wetu kinaendelea vizuri kilichobaki ni utekelezaji tu,”alisema Shime.