Tshishimbi atuliza presha Jangwani

Muktasari:

Papy Kabamba Tshishimbi ni mchezaji pekee wa msimu uliopita wa kigeni aliyebakishwa Yanga msimu huu baada ya wenzake kadhaa kutimka akiwamo Heritier Makambo, Amissi Tambwe, kipa Klaus Kindoki na Thaban Kamusoko.

WAKATI mashabiki wa Jangwani preha zao zikiwa juu kwa kutoridhika na chama lao, ambayo jana lilipata ushindi mwembamba ugenini mjini Mtwara dhidi ya Ndanda, nahodha wa timu hiyo, Papy Kabamba Tshishimbi amewatuliza na kuwaambia timu yao bado ina matokeo mengi mazuri na itawashangaza wengi tofauti na wanavyoichukulia.
Yanga imeibuka na ushindi wa bao 1-0 kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona, ukiwa ni wa pili kwao dhidi ya Ndanda katika uwanja huo na Tshishimbi akiuzungumzia alisema haikuwa kazi rahisi wao kuupata pamoja na kutengeneza nafasi nyingi za kufunga.
Alisema mchezo ulikuwa mgumu kwa kila upande kutokana na timu zote mbili kuwa katika nafasi mbaya kwenye msimamo wa ligi huku akibainisha kuwa kosa moja walilolifanya wapinzani wao ndio walilitumia kuwadhibu.
"Tumetoka katika maumivu kwa kupoteza mchezo muhimu wa kufuzu hatua za makundi kombe la Shirikisho isingekuwa rahisi kurudia tena makosa, tulipambana dakika zote ili tuweze kupata matokeo tunashukuru Mungu tulilifanikisha hilo," alisema.
"Baada ya ushindi huo hatutakiwi kubweteka tunachotakiwa kukifanya ni kukaa karibu na kocha kumuelewa anataka nini na kufanyia kazi kile tunachoelekezwa ili tuweze kufikia mafanikio," alisema nahodha huyo aliyesajiliwa na Yanga msimu uliopita akitokea Mbabane Swallows.