Teknolojia ya VAR kutumika fainali za Afcon Misri

Muktasari:

Fainali za Afcon 2019 zitafanyika Misri kuanzia Juni 21 hadi Julai 19, 2019, ikishirikisha timu 24 ikiwa ni mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa mashindano hayo.

Cairo, Misri. Shirikisho la Soka Afrika (CAF) limetangaza litatumia Video Assistance Refereeing technology (VAR) kuanzia hatua ya robo fainali ya mashindano ya Mataifa ya Afrika (AFCON2019).

Fainali za Afcon 2019 zitafanyika Misri kuanzia Juni 21 hadi Julai 19, 2019, ikishirikisha timu 24 ikiwa ni mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa mashindano hayo.

Ukiwa umebakia mwezi na nusu kabla ya kuanza kwa mashindano hayo, CAF imetangaza itatumia teknoloji ya VAR katika mashindano ya AFCON, lakini itaanza kufanya kazi katika raundi ya mtoano.

“VAR itatumika katika fainali za Afcon Misri kuanzia hatua ya robo fainali ya mashindano hayo,” alisema mwenyekiti wa kamati ya waamuzi wa CAF, Souleyman Waberi.

Hiyo inamaana VAR haitotumika katika mechi za hatua ya makundi pamoja na raundi ya 16 bora na itatumika pekee katika robo fainali ya mashindano hayo.

Hii si mara ya kwanza kwa VAR kutumika katika soka la Afrika, mara ya kwanza ilijaribiwa katika fainali za Mataifa ya Afrika kwa Wachezaji wa ndani (CHAN2018) nchini Morocco, pia ilitumika katika fainali ya Ligi ya Mabingwa pamoja na Kombe la Shirikisho Afrika.