Straika Kenya apaota Msimbazi

STRAIKA Marcel Boniventure wa Simba anayekipiga kwa mkopo katika kikosi cha AFC Leopards ya Kenya, amesema bado ndoto yake ni kukipiga kwenye klabu yake ya Simba.

Marcel aliondoka kwenye kikosi hicho baada ya kukosa nafasi ya kucheza lakini akiwa AFC ameifungia timu hiyo mabao mawili Kombe la FA na moja Ligi Kuu ya Kenya (KPL).

Usajili wa Meddie Kagere ulimfanya mchezaji huyo ambaye aliifungia Majimaji mabao 13 msimu wa 2017/18, kuchomoka Simba kwani ushindani wa namba ni mkubwa.

Akizungumza na Mwanaspoti, Marcel alisema “Kwa muda ambao nimekaa huku naamini kabisa nikirejea baada ya mkataba wangu wa mkopo kumalizika nitapambana kucheza na wachezaji waliopo Simba kwani ni sehemu sahihi kwangu kipindi hiki,”

Alisema anafahamu changamoto ya namba kiasi cha kuwafanya wachezaji wengine kutocheza kipindi hiki lakini amekuwa akijiandaa kwaajili ya kukabiliana na changamoto hiyo.

“Mkataba wangu wa mkopo unaisha Desemba kwahiyo bado nitakuwa mchezaji wa Simba, kikubwa ambacho nakifanya mimi kuzidi kupambana niwe vizuri zaidi kwa muda huu uliobaki kabla ya kurejea,” alisema.

Mshambuliaji mwingine aliyetolewa kwa mkopo ni Mohammed Rashid ambaye alitimkia KMC.