Sir Alex Ferguson awapa tano Liverpool
Muktasari:
- Ferguson ndiye kocha anayeongoza kwa kutwaa idadi kubwa ya mataji ya Ligi Kuu ya England ambapo chini yake, Manchester United imetwaa taji hilo mara 13
London, England. Kocha na mchezaji wa zamani wa Liverpool, Kenny Dalglish amefichua kuwa kocha wa zamani wa Manchester United, Sir Alex Ferguson amewatumia ujumbe wa pongezi baada ya Liverpool kutangaza ubingwa wa Ligi Kuu England (EPL) juzi Alhamisi.
Ushindi wa mabao 2-1 ambao waliupata Chelsea dhidi ya Manchester City uliifanya Liverpool itangazwe rasmi kuwa bingwa wa taji hilo msimu huu huku wakiwa na michezo saba mbele yao kabla ya msimu kumalizika.
Liverpool wanaongoza msimamo kwa tofauti ya pointi 23 ambazo hakuna klabu inayoweza kuzifikia.
Lakini licha ya uhasama mkali uliopo baina ya Liverpool na United, Ferguson aliweka kando hilo na kutoa pongezi ambazo Dalglish amekoshwa nazo.
"Amewasiliana nasi kusema hongereni - haupo vitani!" Dalglish alinukuliwa akisema.
"Kuna ushindani kati ya maadui wote wa zamani, lakini mwishoni mwa mwaka unapeleka ujumbe wa pongezi kusema umefanya vizuri.
"Hiyo inaendelea na ni pongezi nzuri. Unaweza kuwa mpinzani lakini unapaswa kuwa na ujasiri wa kutuma ujumbe wa pongezi.
"Watu ambao umekuwa ukishindana na maisha yako yote katika mpira wa miguu, wangetamani ni wao wenyewe walioshinda, lakini wanajivunia kuwaheshimu watu wengine pia,” alisema Dalglish
Makocha hao wawili wa zamani, walikuwa na tabia za kutupiana maneno wakati wakishindana katika mikiki ya Ligi Kuu ya England