Simba yapewa wababe wa Azam, Kessy awangojea

Muktasari:

Mara ya mwisho kwa Simba kukutana na timu kutoka Kusini mwa Afrika kwenye mashindano ya kimataifa ilikuwa ni 2003, ambapo walitolewa kwa matokeo ya jumla ya mabao 5-0 na Recreativo Do Libolo ya Angola ambapo walifungwa 1-0 hapa Tanzania kabla ya kufungwa 4-0 ugenini.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeipa mfupa mgumu Simba kwenye mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao baada ya kuwapanga dhidi ya Mbabane Swallows kutoka nchi  ya Utawala wa Eswatini zamani ikijulikana kama Swaziland.
Timu hiyo ndio iliwahi kuwatupa nje Azam FC kwenye mashindano ya Kombe la Shirikisho Afrika katika raundi ya kwanza mwaka 2017.
Katika ratiba iliyotolewa na CAF leo, Simba itaanzia nyumbani kuwakabili Swallows kati Novemba 27 hadi 28 na baada ya hapo itacheza ugenini kati ya Disemba 4 na 5 mwaka huu.
Mshindi wa mechi mbili baina ya timu hizo atakutana na mshindi wa mchezo baina ya Nkana Red Devils ya Zambia na UD Do Songo ya Msumbiji kusaka timu itakayofuzu hatua ya makundi.
Wakati hali ikiwa hivyo kwa Simba, mabingwa wa Zanzibar, JKU wenyewe wamepangwa kukutana na Al Hilal ya Sudan na mshindi wa mechi atakutana na mshindi wa mechi baina ya APR ya Rwanda na Club Africain ya Tunisia.
Wawakilishi wa Tanzania  kwenye Kombe la Shirikisho Afrika, Mtibwa Sugar wenyewe wamepangwa kukutana na Northern Dynamo ya Shelisheli na mshindi wake atakutana na KCCA ya Uganda.
Nao Zimamoto wamepangwa kuanza dhidi ya Kaizer Chief ya Afrika Kusini na kama watapenya basi watakutana na mshindi wa mechi itakayokutanisha timu za El  Geco ya Madagascar na Deportivo Unidado ya Guinea ya Ikweta