Simba ni do or die kwa AS Vita

Muktasari:

Katika msimamo huo wa Kundi D, vinara ni JS Saoura yenye pointi nane, Al Ahly ni ya pili ina pointi saba ambazo ni sawa na AS Vita huku Simba ikishika mkia na pointi sita.

Dar es Salaam. Wakati yakiwa yamebaki masaa machache Simba kuwavaa AS Vita Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, kipa wa Wekundu hao wa Msimbazi, Aishi Manula wametamba kikosi chao kitaandika historia mpya katika mchezo huo.
Simba itacheza mchezo huo wa kukamilisha idadi ya mechi sita za Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya makundi ambapo zimepangwa Kundi D, pamoja na Al Ahly ya Misri na JS Saoura ya Algeria.
Mlinda mlango wa Simba, Aishi Manula amesema wana kila sababu ya kuhakikisha Simba inaandika historia hiyo kwa kuingia hatua ya robo fainali.
"Kitu kikubwa ninachowaomba mashabiki wote wa Simba kujitokeza kwa wingi Uwanja wa Taifa kwa ajili ya kuisapoti timu yetu tuweze kufanya vizuri katika mchezo wetu,"alisema Manula.
Amesema, kama Simba itafanya vizuri katika mashindano hayo makubwa, itafanya mpira wa Tanzania kukua na kujulikana ulimwenguni.
"Kufanya kwetu vizuri Tanzania itatangazika na kujulikana. Kufanya kwetu vizuri itakuwa chachu na hamasa kwa timu yetu kama kauli mbiu inavyosema Do or die,"alisema Manula.
Timu zote nne zina nafasi ya kusonga mbele hatua ya robo fainali na zitakazopita ni mbili tu.