Simba yaongeza nguvu fainali ya Azam

Muktasari:

Wachezaji watakaowasili kuongeza nguvu ni Haruna Niyonzima, Shiza Kichuya, Rashid Juma pamoja na Mzamiru Yassin.

Muda mchache baada ya Azam kutua kisiwani Pemba, Simba nao waliingia na kutamba kuongeza wachezaji wazoefu kwenye fainali hiyo itakayochezwa jioni ya leo Jumapili uwanja wa Gombani.
Kocha mkuu wa timu ya vijana ya Simba ambaye amrkabidhiwa jukumu la kuhakikisha wanatwaa ubingwa wa Kombe la Mapinduzi, Nico Kiondo alisema kutokana na umuhimu wa mechi hiyo ataongeza wachezaji wazoefu.
Wachezaji watakaowasili kuongeza nguvu ni Haruna Niyonzima, Shiza Kichuya, Rashid Juma pamoja na Mzamiru Yassin.
Kiondo alisema "Mzamiru anatakiwa kuja ingawa kuna taarifa zingine zinasema hawezi kuja hivyo tunasubiri mpaka wafike ili tujue kama yupo ama hayupo, ila tumejinga Azam ni timu kubwa na wachezaji wazuri wanao.
"Ni mechi muhimu kwetu na sisi tunahitaji ubingwa hivyo kutakuwepo na mabadiliko kwenye kikosi cha leo hasa kwa kuongeza wazoefu, vinginevyo wachezaji wote wapo vizuri," alisema Kiondo