Simba Queens, Yanga Princess zachemka vibaya kwa maafande

Muktasari:

  • Mwanahamisi ametamba atahakikisha raundi ya pili mechi zilizosalia zinamwingiza kwenye ushindani wa kuzifumania nyavu.

SIMBA Queens na Yanga Princes zimeendelea kuburuzwa kwenye msimamo wa wafungaji wa Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania Bara, huku JKT Queens ikiwa inaongoza kutoa vinara wa kuzifumania nyavu.

Kinara wa mabao ni Fatuma Mustapha wa JKT Queens (23), akifuatia na Asha Rashid ‘Mwalala’ (ana mabao 21), huku Simba Queens ni Mwanahamisi Omary mwenye mabao tisa.

Yanga Princess haijatoa mchezaji hata mmoja kwenye tisa bora, licha ya kuwa timu inayoungwa mkono na mashabiki wao kutokana na kutumia uzi wa kijani.

Mwanahamisi ametamba atahakikisha raundi ya pili mechi zilizosalia zinamwingiza kwenye ushindani wa kuzifumania nyavu.

“Tunatazamwa Simba Queens na Yanga Princes kuwa mfano kwa timu nyingine kwa sababu ya timu za wanaume zilivyo na ushindani na zina mashabiki wengi, binafsi nitapambana kadri nitakavyoweza kuingia kwenye ushindani wa kuzifumania nyavu ingawa nafanya majukumu mengi uwanjani,” alisema.

Kwa upande wa Fatuma alisema kadri mechi zinavyochezwa ndivyo anavyotamani kufunga zaidi.