Simba Queens, Yanga Princess kupigwa Uhuru

Muktasari:

Awali mchezo huo ilikuwa uchezwe uwanja wa Mo Simba Arena, lakini umeamishwa na utachezwa uwanja wa Uhuru.
 

MECHI ya Ligi Kuu ya Wanawake kati ya Simba Queens na Yanga Princess imebadilishiwa Uwanja kutoka Mo Simba Arena na sasa itacheza Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

Awali ilikuwa inajulikana kuwa ingechezwa huko Bunju, lakini kutokana na sababu ambazo hazikuwekwa wazi taarifa za  kubalishwa zilitoka hapo jana Alhamisi jioni.

Akizungumza na Mwanaspoti Online, kocha wa Yanga Princess, Edna Lema, amesema jambo hilo kwao halijaathiri chochote kwenye mbinu zao, kwani walijiandaa kucheza popote.

"Taarifa tumepokea jana mchana na hatujaathirika kivyovyote kwani tulijiandaa kucheza popote, hata kama tungepelekwa Chamazi Complex, Karume ama wakirudisha huko huko Mo Arena, bado tungeenda kucheza tu" amesema.

" Mpaka sasa kikosi kipo sawa sawa na tunaendelea vizuri, pia hakuna majeruhi kwa wachezaji wote"ameongeza.

Juhudi za kuwatafuta viongozi wa Simba, ili kuzungumzia mabadiliko hayo ya uwanja ziligonga mwamba baada ya simu zao kutokuwa hewani.

Mchezo huo unatarajia kucheza saa leo Ijumaa 10:00 jioni, unatajwa kuwa ni mchezo wa kisasi, baada ya Yanga kupoteza mechi tatu zilizopita kwa vipigo vya aibu, mchezo wa kwanza alifungwa bao 7-0, wa pili akafungwa bao 5-1 na msimu huu amechezea bao 3-1.

Mpaka sasa Simba Queens wana pointi 35 wamecheza mechi 14 wanashika nafasi ya pili baada ya jana Alhamisi JKT Queens kushinda mechi yao dhidi ya Mlandizi bao 5-2 na kupanda kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo.

Yanga wao wanahsika nafasi ya tano wakiwa na pointi 23 wamecheza mechi 14.