Simba: Alikuja AS Vita akakaa, Al Ahly akakaa na Sevilla atakaa

Muktasari:

  • Sevilla ni mabingwa wa kihistoria wa mashindano ya Europa League wakitwaa taji hilo mara tano

Dar es Salaam. Katika kile kinachoonekana kuongeza hamasa ya mchezo wa kimataifa wa kirafiki kati ya Simba dhidi ya Sevilla kesho, Mtendaji Mkuu wa Simba, Crescentius Magori ametamba timu yake itaibuka na ushindi kwenye mchezo huo.

Akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari leo, Magori alisema wanatambua ubora na ukubwa wa Sevilla, lakini wamejipanga kuhakikisha wanawashangaza kwa kuwafunga kesho.

"Sevilla ni timu kubwa. Imeanzishwa muda mrefu na imetwaa ubingwa wa Europa. Sisi kama Simba ni klabu ya historia na klabu ya rekodi na tuna furaha kupewa nafasi ya kuandika historia ya kucheza na Sevilla inayokuja kwa mara ya kwanza.

Kama mnavyofahamu Simba imefanya mabadiliko ya uendeshaji wake na kama mlivyoona mabadiliko hayo yameleta mafanikio makubwa.

“Ninachoahidi kesho utapigwa mtanange ambao haujawahi kutokea hapa Tanzania. Kwa sauti ya Ofisa Habari wetu, Haji Manara, niseme alikuja Vita akakaa, Al Ahly akakaa na Sevilla naye atakaa," alisema Magori.

Magori alisema Simba inaamini ujio wa Sevilla utakuwa msaada mkubwa kwao kwenye upande wa utawala.