Sikia hii kitu ya Griezmann

Muktasari:

Lakini, kinachoelezwa ni kwamba Griezmann hakwenda kwenye kikosi cha Barcelona kwa sababu si chaguo la mashabiki wa timu hiyo.

BARCELONA, HISPANIA

ALIYEKUWA rais wa klabu ya Barcelona, Joan Laporta amesema kwamba miamba hiyo ya Nou Camp inapaswa tu kuachana na mpango wa kumsajili supastaa wa Atletico Madrid, Antoine Griezmann.

Griezmann aliweka mambo wazi wakati alipokiri kuipenda Barcelona mwaka jana kwenye dirisha la uhamisho wa majira ya kiangazi wakati staa huyo alipokuwa akihusishwa na mpango wa kutimkia Nou Camp kabla ya dili hilo kushindwa kufanikiwa na Mfaransa huyo kubaki Atelico.

Lakini, kinachoelezwa ni kwamba Griezmann hakwenda kwenye kikosi cha Barcelona kwa sababu si chaguo la mashabiki wa timu hiyo.

“Ndio wanaoamua kile wanachodhani ni bora. Ila ninachokiamini ni kwamba mashabiki wengi hawamtaki Griezmann,” alisema Laporta.

“Hii ni kwa sababu ya bei anayouzwa. Amekuzwa sana na kwamba ninachokiamini kuna wachezaji wengine wenye uwezo mkubwa wa kucheza nafasi ya Griezmann.

“Wachezaji wanataka kuja Barcelona, yeye ni mchezaji mzuri lakini nandhani alikuwa na nafasi hiyo mwaka jana akashindwa kuitumia, ameamua kucheza mchezo wa kusumbuana na Barcelona.”