Sibomana, Molinga waamsha mzuka Kirumba

Muktasari:

Baada ya bao hilo, Molinga ndio kama vile alipewa ruhusa sasa ya kuchezea mpira atakavyo, nyota huyo aliwapa mzuka mashabiki kwa kupiga pasi za visigino na kuachia shuti ndani ya 18 ambayo yote yaliokolewa na Ntala.

NYOTA wa Yanga, Patrick Sibomana na David Molinga wamewapa mzuka mashabiki wao kipindi cha kwanza baada ya kufunga bao na kuonyesha udambwiudambwi wa kila namna walipokuwa na mpira.

Ilikuwa hivi, dakika 15 za kwanza, Alliance na Yanga walikuwa wanacheza kwa kushambuliana kwa zamu, jambo hilo lilipelekea mashabiki kuwa kimya sana katika Uwanja wa CCM Kirumba wakishuhudia mtanange huo wa Ligi Kuu .

Lakini ukimya huo ulikatika ghafla dakika ya 25 ya mchezo baada ya Sibomana kukwamisha mpira wavuni ambao ulimshinda kipa wa Alliance, Andrew Ntala na kupelekea timu yake kuongoza bao 1-0.

Baada ya bao hilo, Molinga ndio kama vile alipewa ruhusa sasa ya kuchezea mpira atakavyo, nyota huyo aliwapa mzuka mashabiki kwa kupiga pasi za visigino na kuachia shuti ndani ya 18 ambayo yote yaliokolewa na Ntala.

Licha ya kufungwa bao hilo na kufanya mashambulizi ya mara kwa mara langoni kwa Yanga, Alliance walishindwa kupata bao kipindi cha kwanza jambo ambalo likasababisha waende mapumziko wakiwa kichwa chini.