Shime akana kugomea medali

Muktasari:

Mabao mawili ya straika wa timu ya Taifa ya Kenya (Harambee Starlets), Jentrix Shikangwa yalitosha kupeleka kilio kwa mashabiki wa Tanzania waliofurika kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi. 

WAKATI wa kutoa medali za mshindi wa pili wa mashindano ya Cecafa Wanawake kwa timu ya Tanzania Bara 'Kilimanjaro Queens' Kocha Mkuu Bakari Shime na msaidizi wake, Edna Lema hawakuchukua.
Hata hivyo, wenyewe wameibuka na kutolea ufafanuzi suala hilo la kutoonekana kuchukua medali hizo.
Shime, ambaye kikosi chake kilichapwa mabao 2-0 kwenye mchezo wa fainali na timu ya Taifa ya Kenya, Harambee Starlets, jana Jumatatu ikiwa ni mara ya kwanza kwa michuano hiyo kufanyika nchini Tanzania.
"Sikugomea, ukweli ni kuwa medali zilikuwa 25 na sisi yaani mimi pamoja na benchi langu la ufundi, tulizidi hiyo idadi hivyo, nilitoa nafasi kwa wengine kupata medali hizo," alisema Shime.
Kwa upande wake, Edna alisema: "Sababu kubwa ni uchache wa medali, zilikuwa 25 na sikuona sababu nichukue halafu wengine wakose."
Katika michuano hiyo Tanzania Bara ilianza hatua ya makundi ikiwa Kundi A, pamoja na Burundi, Sudani Kusini na Zanzibar wakati Kundi B, lilikuwa na Uganda, Kenya, Djibouti na Ethiopia.
Kilimanjaro Queens ilishinda mechi zote za makundi na na kupoteza kwenye fainali mbele ya Harambee Starlets.
Hata hivyo, kupoteza mchezo huo kumeinyima fursa Kilimanjaro Queens kubeba taji hilo kwa mara ya tatu baada ya kufanya hivyo, mwaka 2016 na 2018.