Sarri: Willian huko Chelsea

Muktasari:

Nyota wa Chelsea, Mbrazil William anasema, anavurugwa na Kocha Maurizio Sarri ndani ya Stamford Bridge kutokana na utaratibu wake mpya wa mazoezi ambao unambana na kumfanya ashindwe kufurahia maisha na familia yake.

LONDON, ENGLAND. STAA wa Chelsea, Mbrazili Willian amekiri kuvurugwa na Kocha Maurizio Sarri huko Stamford Bridge.
Willian alisema kinachomvuruga kwa sasa ni kutokana na Kocha Sarri kuja na utaratibu mpya wa mazoezi ambao unamfanya asiwe na muda wa kutosha wa kufurahia na familia yake hasa mabinti zake.
Kocha Sarri baada ya kutua tu Chelsea kuchukua mikoba ya Antonio Conte mwishoni mwa msimu uliopita amebadili mfumo wa mazoezi wa timu hiyo, akiwataka wachezaji wake kufanya mazoezi jioni na si asubuhi tena kama ilivyokuwa awali.
Jambo hilo linamfanya Willian adai linamnyima nafasi ya kufurahia mambo na familia yake kwa sababu nyakati nzuri za kufanya hivyo ni jioni, lakini kwa sasa muda huo unapaswa kuwa mazoezini, hivyo amevurugwa sana.
Willian alisema: “Ni wazi, napenda kufanya mazoezini asubuhi kwa sababu baada ya hapo unakuwa na muda wa kuwa na familia yako. Lakini, ukifanya mazoezini jioni, ukirudi nyumbani unakaa kidogo tu na wanao, mnakula, wanakwenda kulala.
“Basi nawaona kwa muda mfupi sana mabinti zangu, ndio maana napenda tufanye mazoezi asubuhi."