Samatta uso kwa uso na Pepe

Muktasari:

  • Mchezo wa leo wa Europa Ligi kati ya KRC Genk dhidi ya Beşiktaş, utawakutanisha kwa mara ya kwanza nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta dhidi ya  Pepe.

Dar es Salaam. Mshambuliaji wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Samatta anatarajiwa leo  kukutana uso kwa uso na beki wa zamani wa Real Madrid, Pepe kwenye mchezo wa Europa Ligi.

Samatta anayeichezea KRC Genk ya Ubelgiji atakuwa  na kibarua kizito mbele ya Pepe ambaye alikosekana kwenye mchezo uliopita ambao  Beşiktaş ilipoteza nyumbani  kwa mabao 4-2.

Kukosekana kwa Pepe  kwenye mchezo uliopita ambao Samatta alifunga mara mbili, kulitokana na majeruhi ambayo yalikuwa yakimsumbua kwa siku 17, kuanzia Oktoba 13 hadi 30.

Beki huyo mwenye uzoefu wa kutosha aliikosa michezo mitatu ya Beşiktaş  ambayo waliishia kupoteza miwili mbele ya Goztep kwa mabao 2-0 kwenye Ligi  na Europa dhidi ya Genk kwa mabao 4-2 na wakashinda mara mmoja dhidi ya Rizespor kwa mabao 4-1.

Mara baada ya Pepe  kurejea kwenye mchezo uliopita  dhidi ya İstanbul Başakşehir wakajikuta wanapoteza kwa mara ya tatu kwenye Ligi msimu huu wa 2018/19.

Kama KRC Genk itafanikiwa kuibuka na ushindi kwenye mchezo huo wa raundi ta nne, watakuwa katika  mazingira mazuri ya kufuzu kwenda kwenye mzunguko wa timu 32 bora.

KRC Genk wataingia kwenye mchezo huo utakaopigwa majira ya saa 2:55 kwa saa za Afrika Mashariki  wakimtegemea Samatta ambaye amekuwa kwenye kiwango bora cha ufungaji

Nahodha huyo wa Taifa Stars, msimu huu wa 2018/19 amefunga jumla ya mabao 19 kwenye mashindano yote kwenye idadi hiyo 10 ni kwenye Ligi ndani ya michezo 13, tisa ni kwenye Europa ndani ya michezo nane.