Samatta uso kwa uso na Pepe
Muktasari:
- Mchezo wa leo wa Europa Ligi kati ya KRC Genk dhidi ya Beşiktaş, utawakutanisha kwa mara ya kwanza nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta dhidi ya Pepe.
Dar es Salaam. Mshambuliaji wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Samatta anatarajiwa leo kukutana uso kwa uso na beki wa zamani wa Real Madrid, Pepe kwenye mchezo wa Europa Ligi.
Samatta anayeichezea KRC Genk ya Ubelgiji atakuwa na kibarua kizito mbele ya Pepe ambaye alikosekana kwenye mchezo uliopita ambao Beşiktaş ilipoteza nyumbani kwa mabao 4-2.
Kukosekana kwa Pepe kwenye mchezo uliopita ambao Samatta alifunga mara mbili, kulitokana na majeruhi ambayo yalikuwa yakimsumbua kwa siku 17, kuanzia Oktoba 13 hadi 30.
Beki huyo mwenye uzoefu wa kutosha aliikosa michezo mitatu ya Beşiktaş ambayo waliishia kupoteza miwili mbele ya Goztep kwa mabao 2-0 kwenye Ligi na Europa dhidi ya Genk kwa mabao 4-2 na wakashinda mara mmoja dhidi ya Rizespor kwa mabao 4-1.
Mara baada ya Pepe kurejea kwenye mchezo uliopita dhidi ya İstanbul Başakşehir wakajikuta wanapoteza kwa mara ya tatu kwenye Ligi msimu huu wa 2018/19.
Kama KRC Genk itafanikiwa kuibuka na ushindi kwenye mchezo huo wa raundi ta nne, watakuwa katika mazingira mazuri ya kufuzu kwenda kwenye mzunguko wa timu 32 bora.
KRC Genk wataingia kwenye mchezo huo utakaopigwa majira ya saa 2:55 kwa saa za Afrika Mashariki wakimtegemea Samatta ambaye amekuwa kwenye kiwango bora cha ufungaji
Nahodha huyo wa Taifa Stars, msimu huu wa 2018/19 amefunga jumla ya mabao 19 kwenye mashindano yote kwenye idadi hiyo 10 ni kwenye Ligi ndani ya michezo 13, tisa ni kwenye Europa ndani ya michezo nane.