Samatta awaomba radhi Watanzania

Muktasari:

Stars iliambulia pointi moja katika mchezo huo uliochezwa Jumamosi kwenye Uwanja wa Mandela, Namboole jijini Kampala na kuweka wazi kuwa hawakuwa na bahati sikuhiyo kwasababu walitengeneza nafasi nyingi.

Dar es Salaam. Nahodha wa timu ya Taifa 'Taifa Stars', Mbwana Samatta amesema bado anaumizwa na kushindwa kutumia nafasi ya wazi aliyoipata katika mchezo wao wa kufuzu kushiriki Afcon dhidi ya Uganda.

Stars iliambulia pointi moja katika mchezo huo uliochezwa Jumamosi kwenye Uwanja wa Mandela, Namboole jijini Kampala na kuweka wazi kuwa hawakuwa na bahati sikuhiyo kwasababu walitengeneza nafasi nyingi.

Alisema amekuwa akifunga mabao yake mengi katika mazingira magumu, lakini Jumamosi alishindwa kutumia nafasi ya wazi aliyoipata akiwa yeye na kipa kitu ambacho kinamuumiza sana hadi sasa.

Samatta alitumia nafasi hiyo kuwaomba radhi mashabiki wake kutokana na kushindwa kuwapa furaha katika mchezo huo ambao ulikuwa ni muhimu kwao kupata ushindi ili kujitengenezea mazingira mazuri katika kundi lao.

"Nafasi niliyoitengeneza juzi nafasi nzuri na ya wazi nilishindwa kufunga tofauti na nafasi nyingine ngumu ambazo nimekuwa nikizipata na kuweza kukwamisha mpira nyavuni naahidi kufanyia kazi kosa nililolionyesha nitapambana kuhakikisha naliondoa katika michezo mingine," alisema Samatta.