Samatta: Tunahitaji ushindi, lazima tushinde
Muktasari:
Samatta alisema kutokana na matokeo ya kwanza yamewapa morali wachezaji wote kupambana zaidi mchezo wa kesho na kushinda kwa kishondo.
NAHODHA wa timu ya Taifa ya Tanzania'Taifa Stars', Mbwana Samatta amesema yeye na wachezaji wenzake wana morali kubwa kuelekea mchezo wa dhidi ya Burundi na anaamini watapata ushindi kwani watakuwa na sapoti kubwa ya Watanzania.
Taifa Stars itakuwa mwenyeji wa Burundi kesho Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa ukiwa ni mchezo wa marudiano wa kuwania kufuzu Fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika Qatar mwaka 2022.
Samatta alisema kutokana na matokeo ya kwanza yamewapa morali wachezaji wote kupambana zaidi mchezo wa kesho na kushinda kwa kishondo.
"Kila mchezaji yuko tayari, morali iko juu sana kutokana na matokeo ya mechi ya kwanza na tunatarajia matokeo ya Jumapili yatakuwa mazuri kwa sababu tunacheza nyumbani na tuna uhakika Watanzania wengi watajitokeza kutusapoti.
"Nguvu ambayo tutaionyesha pamoja kuanzia wachezaji, benchi la ufundi na mashabiki na imani matokeo yatakwa mazuri"alisema Samatta.
Hata hivyo Samatta amewataka Watanzania kuweka ushabiki wa klabu na mambo mengine pembeni na kila mmoja kuisapoti timu ya Taifa kwani timu hiyo ni ya kila Mtanzania.
"Wanaoweza kuja uwanjani Jumapili wafike kwa wingi ili kuisapoti timu yao na wasioweza basi wakunjue moyo kwani hii ni timu ya Watanzania wote. Tuachane na ushabiki usio na faida kwani linapokuja suala la timu ya Taifa ni suala la Kitaifa kila Mtanzania anawajibika linamuhusu moja kwa moja.