Samatta: Misri ni kipimo sahihi kwetu

Muktasari:

  • Katika kombe la Mataifa Afrika ambalo litaanza Juni 21, Taifa Stars wamepangwa kundi C, sambamba na timu za Algeria, Senegal na Kenya.


KIPIGO cha bao 1-0 walichokipata Taifa Stars dhidi ya Misri juzi Alhamis kimeelezwa kwamba ni kipimo tosha kwao ambapo Nahodha wa timu hiyo Mbwana Samatta amesema matokeo hayo yamewapa mwelekeo kuelekea Fainali za Afcon.
Fainali hizo zinatarajia kuanza Juni 23 nchini Misri ambapo Stars imepangwa kundi moja na timu ya Algeria, Kenya na Senegal watakaocheza nao mechi ya kwanza.
“Makosa tuliyoyafanya katika mechi hii ya kirafiki yameonwa na benchi la ufundi, matumaini yangu yatafanyiwa kazi kabla ya mashindano kuanza.
“Ukiangalia kundi letu kuna timu kama Senegal, Algeria na Kenya ambao wote si wa kuwabeza kutokana na kuwa na matokeo mazuri katika mashindano mbalimbali ilikuwa lazima tupate mchezo mkubwa kama huu kuona ubora na mapungufu yetu kutokana na maandalizi tunayoyafanya," anasema Samatta.
Keshokutwa Jumapili, Stars itacheza mechi ya pili ya Kimataifa ya kirafiki dhidi ya timu ya Taifa ya Zimbambwe kabla ya Juni 23, kuanza kutupa karata yake ya kwanza dhidi ya Senegal kwenye mashindano.