Safari ya Taifa Stars Afcon, Simba, Yanga tupu kule

Muktasari:

Tanzania mara ya mwisho kufuzu kucheza fainali za Mataifa ya Afrika ilikuwa 1980 nchini Nigeria

Dar es Salaam. KUNA nafasi kubwa kwa Timu ya Taifa ya Tanzania kufuzu kwa fainali za Mataifa huru ya Afrika (Afcon) mwakani pale Cameroon mwakani.

Uwezo wa kufanya hivyo ni mkubwa kuliko kipindi kingine chochote kutokana na kundi tulilipo, kocha Emmanuel Amunike na aina ya wachezaji tulionao katika Stars.

Kutokana na vitu hivyo, Stars haina budi kufuta picha mbaya ya kutoshiriki fainali hizo kwa miaka 38 iliyopita. Yafuatayo ni mambo sita yatakayoikamilisha ndoto hiyo kuwa kweli.

Amunike aheshimiwe

Kocha wa Stars, Amunike ameanza kwa kuonyesha mwanga juu ya kile anachotaka kukifanya na anachotakiwa ni kupewa heshima yake. Hili sio kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) peke yake, bali hata klabu na wadau wengine.

Endapo anachotaka kocha hakitaweza kufanyika kwa kiwango kinachotakiwa tunaweza kuishia kupiga hesabu za vidole.

Matokeo ya Uganda yasahaulike

Kitu muhimu ambacho wachezaji wa Taifa Stars, makocha na hata viongozi wanachotakiwa kukifanya ni kusahau matokeo ya sare tuliyoyapata Jumamosi dhidi ya Uganda.

Hali ilivyo ni kama vile tumemaliza kazi kwa kupata matokeo haya, hilo halitaweza kutupa mafanikio mbele ya safari.

Tunachotakiwa sasa ni kusahau matokeo hayo na kubaki kama morali huku tukitaji mafanikio zaidi ya ushindi katika mechi zilizosalia.

Tutangaze maafa Taifa

TFF inatakiwa kuhakikisha Stars haitakiwi kupoteza michezo miwili iliyobaki nyumbani hata kwa kupata sare.

Hili sio kwa Stars tu hata klabu zetu zimekuwa zikifanya makosa kwa kushindwa kuutumia vizuri uwanja wa nyumbani.

Stars kama ingeshinda mchezo wake dhidi ya Lesotho uliochezwa Uwanja wa Chamazi nafasi ya kwenda Cameroon ingekuwa wazi zaidi ya ilivyo sasa lakini kosa hili halitakiwi kurudiwa dhidi ya Uganda na Carpe Verde.

Stars ikakomae ugenini

Stars itatoka nje mara mbili ikizifuata Lesotho na Carpe Verde. Katika mechi mbili hizi Stars inatakiwa kurudi nyumbani na pointi sita isiwe pointi moja au kukosa kabisa.

Nguvu ya Stars kutoka na pointi sita ugenini ipo endapo mambo ya kiufundi yatakwekwa sawa. Kitendo cha timu hizo kutoa sare katika mchezo wao wa juzi Jumapili ni ishara ya mafanikio kwa Stars.

Usimba na Yanga tupa kule

Utaifa unatakiwa kupewa kipaumbele na tuweke pembeni itikadi zetu za U-simba na U-yanga.

Tukiendekeza hili litatumaliza mapema. Mashabiki wa Simba, Yanga, Mtibwa na Azam FC wanapoona mchezaji amevaa jezi ya Stars wanatakiwa kumuunga mkono.

Ikumbukwe wengi walidharau safu ya ulinzi ya Stars iliyoundwa na mabeki wa Azam, David Mwantika na Aggrey Morris na kuamini timu hiyo ingefungwa mabao mengi dhidi ya Uganda Cranes lakini mambo yalikuwa tofauti. Hilo linapaswa kuwa somo kubwa kwetu kuheshimu uamuzi ya kocha.

Tuujaze Uwanja wa Taifa

Kama ilivyokuwa enzi za Kocha wa Taifa Stars, Marcio Maximo, TFF inatakiwa kuwahamasisha mashabiki kuujaza Uwanja wa Taifa huku wakiwa wamevaa jezi zenye bendera ya taifa.

Tumewaona Waganda walivyoujaza uwanja wao Jumamosi iliyopita.  Hatuna budi kuiga hilo.