Ratiba yamtesa Klopp

Muktasari:

Ushindi dhidi ya Napoli ungewafanya Liverpool kufuzu hatua hiyo ya mtoano, hivyo wasingekuwa na presha katika mchezo wao wa mwisho, lakini sasa watakuwa na shughuli ya kutoa macho kusaka ushindi kwenye mechi 14 itakazocheza ndani ya muda usizofika miezi miwili.

LIVERPOOL, ENGLAND . JURGEN Klopp kichwa kinampasuka kwa sasa baada ya kuona kikosi chake cha Liverpool kimejiongezea ratiba ngumu kwenye mwezi wa Desemba.
Sare ya bao 1-1 dhidi ya Napoli kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya iliyopigwa Anfield Jumatano iliyopita imewafanya Liverpool kujiweka kwenye hali mbaya na sasa kulazimika kuitolea macho mechi yao ya mwisho dhidi ya RB Salzburg ili kufuzu hatua ya mtoano.
Ushindi dhidi ya Napoli ungewafanya Liverpool kufuzu hatua hiyo ya mtoano, hivyo wasingekuwa na presha katika mchezo wao wa mwisho, lakini sasa watakuwa na shughuli ya kutoa macho kusaka ushindi kwenye mechi 14 itakazocheza ndani ya muda usizofika miezi miwili. Hiyo ina maan kwamba kwenye mwezi wa Desemba, Liverpool watakuwa na shughuli pevu na pengine hawatakuwa na muda wa kutosha kufurahia Krismasi.
Mechi 14 ndani ya muda usiofika miezi miwili, hiyo ina maana kwamba Liverpool watalazimika kucheza mechi moja katika kila baada ya siku tatu au nne kwa wiki saba mfululizo.
Liverpool wapo kwenye michuano yote, Ligi Kuu England, Kombe la Ligi, Kombe la FA na Ligi ya Mabingwa Ulaya na watacheza pia Klabu Bingwa Dunia, michuano ambayo kila moja itakuwa na mechi za kucheza ndani ya Desemba.
Mechi yao ya Kombe la Ligi dhidi ya Aston Villa, ambayo itakuwa ya robo fainali, imetofautiana kwa saa 24 tu na ile ya Klabu Bingwa Dunia watakayopaswa kuchezwa huko Qatar. Jambo hilo linamfanya Klopp kulazimika kutumia vikosi viwili tofauti kwenye mechi hizo mbili, kimoja kikiwa cha wachezaji makinda, lakini hatakuwa na ujanja kwenye mchezo dhidi ya RB Salzburg, kwa sababu atahitaji mastaa wake wote kupata matokeo ya kuwaingiza kwenye hatua ya mtoano.
Kwa kuanzia sasa hadi Januari 2, Liverpool itakuwa kwenye mchakamchaka mkali katika kuhakikisha inajiweka salama kwenye michuano yote ili kubeba mataji yote, hasa la Ligi Kuu England ambalo wamesubiri kwa miaka 30.