Pogba achana Jose

Muktasari:

Mourinho alimtuhumu Pogba na kumwita kirusi anayewaharibu wachezaji wengine kwenye kikosi hicho, jambo ambalo kiungo huyo wa Ufaransa ameamua kujibu na kusema hataki kufanywa mbuzi wa kafara pale Man United inapofanya ovyo.

MANCHESTER, ENGLAND.KIUNGO Paul Pogba amemwambia Kocha Jose Mourinho aache kumshushia lawama juu ya matatizo yanayoikabili Manchester United kwa sasa.

Pogba na kocha wake huyo wameripotiwa kupishana Jumamosi iliyopita kwenye vyumba vya kubadilishia huko St Mary’s baada ya sare ya 2-2 baina ya Southampton na Man United mchezo wa Ligi Kuu England.

Mourinho alimtuhumu Pogba na kumwita kirusi anayewaharibu wachezaji wengine kwenye kikosi hicho, jambo ambalo kiungo huyo wa Ufaransa ameamua kujibu na kusema hataki kufanywa mbuzi wa kafara pale Man United inapofanya ovyo.

Mourinho alisema mengi ikiwamo kukiambia kikosi kizima wanapokuwa uwanjani wajaribu kuwafikiria wachezaji wenzao na kama hawapo tayari kujitolea kwa asilimia 100, basi wajiweke tu pembeni.

Majibizano hayo mapya ya wawili hao yamekuja katika kipindi Man United inakabiliwa na mechi ngumu kabisa na usiku wa jana Jumatano ilitarajia kumenyana na Arsenal huko Old Trafford.

Kabla ya mechi hiyo, Man United imevuna pointi mbili kati ya tisa ilizozibeba kwa siku za karibuni. Mourinho amezungumzia timu sita zilizopo juu kwenye msimamo huenda zikabaki hivyo hivyo hadi msimu unamalizika, huku wao kitu ambacho wana uwezo nacho ni kuivuka Everton tu.