Pluijm asafisha nyota ya dogo

Muktasari:

  • Mshambuliaji huyo kwa upande wake alisema kuna mambo yanawekwa sawa na anaweza kufuata nyazo za Farid Mussa na Shaaban Chilunda kwa kucheza soka la kulipwa nje ya Tanzania.

KOCHA wa Azam, Hans van der Pluijm amesema mshambuliaji wake kinda, Yahya Zayd anaweza kufuata nyayo za Saimon Msuva ambaye alipita kwenye mikono yake kabla ya kusajiliwa na Difaa El Jadida ya Morocco.

Hans alisema juhudi ni miongoni mwa mambo ambayo yalikuwa yakimbeba Msuva na kumtofautisha na wachezaji wengine ambao alikuwa nao kwenye kikosi cha Yanga.

“Sai alikuwa akifanya vizuri kwa kucheza kutokana na nafasi, mpira wangu unategemea pia maeneo ya pembeni kama tutamiliki kwa kiasi kikubwa inamaana kutakuwa na mianya kwenye maeneo hayo, Msuva alikuwa akifanya vyema kwenye hilo.

“Siwezi kuwafananisha na Zayd lakini naona na yeye anauwezo wa kupiga hatua kutokana na umri wake. Anauwezo wa kuimarika zaidi,” alisema Mholanzi huyo.

Julai ya mwaka huu, Zayd mwenye mabao matatu Ligi Kuu Bara, alikwenda Afrika Kusini kufanya majaribio ya wiki kadhaa kwa ajili ya kujiunga na Bidvest Wits inayoshiriki Ligi Kuu nchini humo.

Mshambuliaji huyo kwa upande wake alisema kuna mambo yanawekwa sawa na anaweza kufuata nyazo za Farid Mussa na Shaaban Chilunda kwa kucheza soka la kulipwa nje ya Tanzania.

Chilunda na Farid ni zao la Azam ambao kwa nyakati tofauti walipata fursa ya kujiunga na CD Tenerife ya Hispania.