Paris Saint-Germain yazidi kuikomalia saini ya Dele Alli

 TOTTENHAM Hotspur imekataa ofa ya Paris St-Germain ya Pauni 1.5 milioni, ili kumtoa kiungo wake na timu ya Taifa ya England, Dele Alli kwa mkopo katika dirisha hili la usajili wa majira ya kiangazi.

Alli ambaye hapati nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza cha Spurs chini ya Jose Mourinho mara kwa mara, amewahi kuhusishwa na dili la kutaka kujiunga na miamba hiyo ya Ufaransa miezi kadhaa iliyopita lakini mambo hayakwenda sawa.

Licha ya ofa yao kukataliwa PSG inataka kuwasilisha ofa nyingine kwa ajili ya mchezaji ambaye hapo awali ilikuwa tayari kutoa zaidi ya Pauni 60 milioni ili kumsainisha moja kwa moja.

Mkataba wa Alli, 24, unatarajiwa kumalizika mwaka 2024 thamani yake katika soko la usajili ni Euro 64 milioni. Hata hivyo, katika msimu uliopita mchezaji huyo aling’ara kikosini akifunika pengo lililoachwa na Harry Kane aliyekuwa majeruhi muda mrefu.