Pamba yataka kurudia enzi zileee

Kikosi cha Pamba FC kikijifua katika moja ya mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza (FDL),timu hiyo inajitupa uwanjani kesho Jumatano kuwakabili Mbeya kwanza katika mchezo wa mchujo'Palay Off'.

Muktasari:

  • Kisaka alisema mchezo huo ni muhimu sana kwao katika harakati zao za kusaka nafasi ya kucheza Ligi Kuu msimu ujao, hivyo watapambana kufa au kupona kutafuta ushindi.

MWANZA.UNAIKUMBUKA ile Pamba ya Mwanza iliyotikisha nchi ikifahamika kwa jina la ‘TP Lindanda’ au ‘Wana Kawekamo’? Umelimisi kwenye Ligi Kuu ya Bara lile chama lao matata lililowahusisha kina George Masatu, Fumo Felician, Nteze John ‘Lungu’, Madata Lubigisa na Paul Rwechungura?

Basi hawa hapa vijana wapya wa kizazi cha sasa, wanapambana kuirudisha historia.

Chini ya kocha wao, Ally Kisaka, Pamba wamedhamiria kushinda mechi yao ya mchujo (Play-Off) dhidi ya Mbeya Kwanza ili kujiweka katika mazingira mazuri ya kucheza Ligi Kuu msimu ujao.

Pamba ambayo ilimaliza Ligi Daraja la Kwanza katika nafasi ya pili kwa pointi 42 kundi B, itakuwa ugenini kuwakabili wapinzani hao walioshika nafasi ya tatu kwa alama 38 kwenye kundi A.

Katika ligi hiyo iliyomalizika hivi karibuni, timu za Namungo FC (kundi A) na Polisi Tanzania (kundi B) ndizo zilizofuzu moja kwa moja kucheza Ligi Kuu msimu ujao.

Kisaka alisema mchezo huo ni muhimu sana kwao katika harakati zao za kusaka nafasi ya kucheza Ligi Kuu msimu ujao, hivyo watapambana kufa au kupona kutafuta ushindi.

“Ni mchezo muhimu sana lakini tunajua hautakuwa mwepesi, kila mmoja anataka kucheza Ligi Kuu kwahiyo atakayeweza kutumia mbinu vizuri ndiye ataondoka na ushindi,” alisema Kisaka.

Naye straika mkongwe wa timu hiyo, Shija Mkina alisema wachezaji wamejiandaa vizuri kukabiliana na wapinzani hao.