Pale Gor Mahia ‘Kogalo’ ni twa twa twa

Muktasari:

Tayari Mwenyekiti wa Gor, Ambrose Rachier kathibitisha kuna baadhi ya wachezaji wameshampa notisi wataondoka.

Nairobi, Kenya.IKO shida! Iko shida buda pale Gor Mahia. Mangira pale kwa sasa hivi ni twa twa twa. Pamoja na kwamba wamegandia kileleni mwa jedwali la ligi kuu wakiwa na mechi mbili za viporo, taarifa zilizopo ni sasa klabu hiyo ipo kwenye tishio la kukimbiwa na wachezaji wake.

Tatizo ni mabingwa hao watetezi wa ligi kuu wamesota hadi wanatia aibu licha ya kulipwa mamilioni ya pesa  kutoka kwa ushiriki wao wa mashindano ya CAF msimu uliopita.

Wanacholia ni kumkosa mdhamini tangu Sportpesa alipoamua kuinua zake. Sasa wachezaji wa Gor hawajalipwa kwa mwezi wa tano sasa ukiwa unaingia.

Tayari Mwenyekiti wa Gor, Ambrose Rachier kathibitisha kuna baadhi ya wachezaji wameshampa notisi wataondoka.

Mmoja wao ni  beki Maurice Onjwang waliyemsajili kutoka Western Stima ambaye Rachier kathibitisha kupokea notisi yake ikimwarifu anapania kuondoka itakapofikia Desemba 6.

Mlinzi huyo anasema kama hatakuwa amelipwa mshahara wake wote kufikia tarehe hiyo basi atalazimika kuvunja mkataba wake na Gor kwa mujibu wa kanuni na sheria za FIFA. Sheri za FIFA zinamruhusu mchezaji kuvunja mkataba wake baada ya miezi mitano kama hajapokea mshahara wake.

Lakini sio yeye tu, yupo pia mmoja wa wachezaji muhimu na tegemeo ambaye kadokeza naye anawazia kusaka ulaji kwingine sababu hali pale Gor imeshindikana. Yeye anapania kuondoka mwishoni mwa mwezi huu ikiwa hawatakuwa wamemlipa.

“Itabidi niinue tu kama hawatanilipa. Nimejitahidi kuvumilia lakini nao wamekuwa na za ovyo sana kila leo ni kunizungusha tu. Najua klabu imesota lakini pia maisha huku nje ni magumu, wanategemea tufanyeje sasa.”

Akitia kauli yake kuhusu taarifa kuwa wachezaji wengine pia wanawazia kujitoa, Rachier anasisitiuza ni Ojwang tu ndiye aliyefuata utaratibu unaofuata kwa kutoa  notisi.

“Ojwang kanipa notisi kwamba ataondoka mwezi ujaoa ikiwa hatutamlipa. Hao wachezaji wengine wanaosemekana nao pia wanataka kuondoka bado hakuna mwingine aliyenipa notisi hivyo taarifa hizo nitazichukuliwa kuwa uvumi tu,” Rachier kasema.