Nyota wa Singida United apania kucheza soka Ulaya

Muktasari:

  • Aliwahi kujiunga na timu ya MFK ya nchini Czech na baadae kwenda Minnesota Fc nchini Marekani, sasa amepania kutumia timu hiyo kuwa kama njia kwenda kucheza ligi kubwa zaidi duniani.

Nyota wa Singida United Ally Ng'anzi awali aliondoka nchini na kwenda kujiunga na timu ya MFK ya nchini Czech na baadae kwenda Minnesota Fc nchini Marekani, sasa amepania kutumia timu hiyo kuwa kama njia kwenda kucheza ligi kubwa zaidi duniani.

Ng'anzi anaendelea vizuri kusakata kabumbu nchini Marekani akitafuta njia ya kucheza soka kwenye ligi kubwa zaidi huko haswa baada ya kuonekana kujituma na kupata nafasi ya kucheza mara kwa mara katika kikosi cha Minnesota FC.

Ng'anzi anayecheza nafasi ya kiungo ndoto zake ni kufika mbali na ataitumia nafasi hiyo ya kucheza soka la kulipwa ambalo anaamini akionesha kiwango kizuri ataonekana na kusajiliwa katika timu nyingine kubwa zaidi.

Mkurugenzi wa Singida United, Festo Sanga alisema amekuwa akiwasiliana mara kwa mara na mchezaji huyo na amekuwa akimuahidi atapambana kadri anavyoweza ili kwenda kucheza katika timu kubwa kama malengo yake yalivyo.

"Mbali ya kuwasiliana nae na kuongea mambo ya msingi ambayo yanaweza kuwa muongozo kwake tumekuwa tukimpa msahada wowote ambao atakuwa anauhitaji kutoka huku nchini haswa katika klabu yake ya Singida ambayo ilimpa nafasi kwa moyo mmoja kwenda nje," alisema Sanga.