Nyoni kupangua kikosi cha Taifa Stars

Muktasari:

  • Nyoni aliumia katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Zimbabwe hivyo alishindwa kuichezea Taifa Stars katika mchezo wa kwanza waliofungwa 2-0 na Senegal.

Cairo, Misri. Habari njema! Ndicho unachoweza kusema baada ya beki wa Taifa Stars, Erasto Nyoni kuanza mazoezi na wenzake jana.

Nyoni aliumia katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Zimbabwe hivyo alishindwa kuichezea Taifa Stars katika mchezo wa kwanza waliofungwa 2-0 na Senegal.

Katika mazoezi ya jana usiku Nyoni alicheza dakika zote katika akioonyesha kurejea katika afya yake.

Kocha msaidizi wa Stars, Hemed Morocco alisema wameridhika na ubora wa sasa wa mkongwe huyo.

Kurejea kwa Nyoni kunaweza kupangua maeneo mawili ya kikosi hicho hasa safu ya kiungo na ile ya ulinzi.

Safu ya kiungo ya Stars haikucheza vyema katika mchezo wa Senegal na kumlazimu kocha Emmanuel Amunike kumtoa Feisal Salum katika dakika za mwisho za kipindi cha kwanza.

Nyoni anamudu kucheza kama kiungo mkabaji nafasi ambayo amekuwa akitumiwa na Kocha Amunike lakini pia beki ya kati.

Stars itakutana na Kenya Alhamisi hii ukiwa ni mchezo wa pili kwa timu zote ambazo zimepoteza kwa idadi sawa mechi za ufunguzi.