Nyie Yanga, msikieni Banana Zorro

Muktasari:

Banana amejitambulisha kama msanii mwenye kipaji cha hali ya juu akitoka kwenye familia ya muziki.

SUPASTAA wa Bongo Flava, Banana Zorro amesema Ligi Kuu Bara ya msimu huu inawapa mashabiki mzuka mkubwa kutokana na ushindani na kwamba, bila atapatikana kulingana na ubora wake uwanjani.

Hata hivyo, Banana ambaye ni shabiki lialia wa Simba, amezungumza na Mwanaspoti  leo Jumanne ya Oktoba 13, 2020 na kufichua kwamba, anatamani kuona Simba ikiandika historia mpya ya kubeba ubingwa kwa mara ya nne mfululizo.

Amesema Simba imefanya usajili wa maana akiwemo Bernard Morrison waliyemnasa kutoka kwa watani zao, Yanga hivyo hana shaka na ubingwa.

"Ujue Yanga ndio inaonekana kusajili zaidi na mashabiki wao wanatamba kuona wamemaliza kazi ndio maana nasema nafurahia ushindani. Hapa tukibeba ubingwa unakuwa na kishindo kikubwa kwani, hawatakuwa na visingizo," amesema Banana na kuongeza:

"Sina maana kwamba misimu mitatu ambayo Simba imechukua sio kwa kishindo, bali nikutokana na maneno maneno ya mashabiki wao wanaoona wamefanya usajili wa funga mwaka, hivyo wakiachwa solombe litakuwa jambo la maana sana na watakuwa na la kujifunza.”

Banana ambaye aliwahi kutamba na ngoma kibao kama Zoba na Mama, amesema ukiachana na kuipenda Simba anaunga mkono juhudi zinazofanywa na nahodha wa Taifa Stara, Mbwana Samatta anayekipiga Fenerbahce ya Uturuki.

"Napenda kazi nzuri, Samatta ni kijana wa Kitanzania ambaye ameonyesha kwamba inawezekana kuwatikisa wazungu, binafsi naheshimu harakati zake na kama kuna watu wanaona anachofanya ni rahisi basi sijui watakuwa na roho gani," amesema