Ninja apelekwa timu B LA Galaxy

Muktasari:

Ninja amesajiliwa timu ya MFK Vyskov ya Jamhuri ya Czech kwa mkataba wa miaka minne na hivi sasa amepewa jezi namba 51.

MCHEZAJI Abdalla Shaibu ‘Ninja’ kutoka Zanzibar ambaye hivi karibuni amejiunga kwa mkopo klabu ya LA Galaxy ya Marekani amepelekwa timu B ya La Galaxy II.

Kwa mujibu wa habari kutoka nchini humo ndani ya timu hiyo inaeleza kuwa baada ya kufanyiwa vipimo vya afya na mambo mengine La Galaxy wamelazimika kumuweka timu ya pili kutokana na kuonekana kuwa anahitaji uzoefu na kuzowea mazingira.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa atakuwa timu B na baadaye atapandishwa kucheza timu kubwa ambayo inashiriki Ligi Kuu ya soka Marekani.

Aidha, taarifa imeeleza kuwa Ninja tayari ameanza mazoezi kwenye timu B ambayo kuna wakati huchanganyika kufanya mazoezi na timu kubwa.

Ninja amesajiliwa timu ya MFK Vyskov ya Jamhuri ya Czech kwa mkataba wa miaka minne na hivi sasa amepewa jezi namba 51.

Taarifa zaidi zimeeleza kuwa Ninja amelazimika kupelekwa timu B baada ya kuonekana hayupo fiti, kwa kutofanya mazoezi kipindi kirefu tangu kumaliza Ligi Kuu ya soka Tanzania Bara msimu uliopita.