Ndikumana mbioni kutua Azam FC

Muktasari:

Ndikumana anajiunga na Azam FC akitokea Lierse S.K. ya Ubelgiji akiwa kama mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba na timu hiyo.

Dar es Salaam. Mshambuliaji wa zamani wa klabu ya Simba, Suleiman Ndikumana yupo mbioni kusaini mkataba wa kuichezea Azam FC.

Ndikumana alicheza Simba mwaka 2007, akiwa pamoja na Emmanuel Gabriel, Juma Kaseja, Musa Hassan Mgosi, Nico Nyagawa na Victor Costa 'Nyumba'.

Ndikumana anajiunga na Azam FC akitokea Lierse S.K. ya Ubelgiji akiwa mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba na timu hiyo.

Rafiki wa karibu wa mchezaji huyo alidai kuwa nyota huyo tayari ameshawasili nchini baada ya mazungumzo na Azam FC kukamilika.

"Sijajua ni lini atasainishwa, lakini mazungumzo kati ya pande mbili yamekamilika na ninahakika msimu ujao tunacheza ligi moja," alisema.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Azam FC, Abdulkarim Amin 'Popat', alisema hilo ni pendekezo la mwalimu, lakini bado hawajamalizana na mchezaji huyo huku akiweka wazi kuwa muda ukifika kataweka wazi.

"Ni kweli mwalimu amemuhitaji mchezaji huyo kwaajili ya msimu ujao wa ligi ikiwa ni sambamba na mashindano ya kimataifa ambayo tunatarajia kuyashiriki bado hatujamalizana naye," alisema Popat.