Nakwambia Abramovich anaipiga bei Chelsea

Muktasari:

  • Tajiri mwingine ni mmiliki wa tiketi za msimu za Chelsea, bilionea Sir Jim Ratcliffe, tajiri mkubwa Uingereza nzima naye yupo kwenye orodha ya watu wanaotaka kuibeba jumla klabu hiyo ya Stamford Bridge.

LONDON, ENGLAND.MMILIKI wa klabu ya Chelsea, Roman Abramovich ameripotiwa kujifungia kwenye mazungumzo na matajiri watatu tofauti kwa ajili ya kuipiga bei timu hiyo.

Ripoti zimekuwa zikidai kwamba bosi huyo wa Chelsea amekuwa kwenye mazungumzo na mataji watatu tofauti, yakiwamo makampuni ya Marekani na Asia kwa ajili ya kuipiga bei timu hiyo.

Tajiri mwingine ni mmiliki wa tiketi za msimu za Chelsea, bilionea Sir Jim Ratcliffe, tajiri mkubwa Uingereza nzima naye yupo kwenye orodha ya watu wanaotaka kuibeba jumla klabu hiyo ya Stamford Bridge.

Hata hivyo, Ratcliffe haoni kama Chelsea ina thamani ya Pauni 2.5 bilioni kama ambavyo anasema Abramovich akitaka kulipwa kiasi hicho kwa ajili ya kuiachia timu hiyo. Mmiliki huyo wa Chelsea ameamua kukiachia pia kile chumba chake pale Stamford Bridge, ambako amekuwa akikaa kutazama mechi, hivyo ni ruhusa kwa mtu mwingine kuanza kukikodi.

Abramovich ana mpango wa kuipiga bei Chelsea baada ya kushindwa kupata kibali cha kuingia Uingereza tangu Mei mwaka jana.